Mahubiri ya Mhashamu Askofu Gervas Mwasikwabhila Nyaisonga wa Jimbo la Mpanda katika
Parokia ya Mtakatifu Gaudence, Makoka siku ya alhamisi 26 Juni 2014 wakati wa ibada
ya Misa Takatifu ya kumwombea na kumuaga Marehemu Sr Crescentia Kapuli wa Shirika
la Watawa wa Bikira Maria Malkia wa Afrika, Jimbo Katoliki Mbeya aliyeuwawa na watu
wanaosadikiwa kuwa ni majambazi siku ya Jumatatu tarehe 23 Juni 2014 katika eneo la
Riverside Jijini Dar Es Salaam.
Ndugu zangu waamini na wageni wetu wote, Tumsifu
Yesu Kristo! ......................................... Milele Amina.
Ndugu
wapendwa, ni vigumu kidogo kutoa mahubiri siku kama ya leo, na hasa ukizingatia tukio
lenyewe linaleta kigugumizi kidogo kutoa mahubiri. Lakini basi tunapohubiri hatuubiri
yale tunayopenda, yale ambayo tunatamani sisi, tunahubiri yale ambayo Roho wa Mungu
anatusukuma tuseme. Basi ninawaalikeni tutafakari machache.
Ndugu wapendwa,
kifo cha Sista Crescentia Kapuli kimewastua wengi na wa mbali na wa karibu wanashindwa
kuamini kama ndivyo hivyo kilivyokuwa na kama sababu ndizo hizo na wengine hawaamini
kama ni kweli amefariki. Lakini ni kweli amefariki na leo hapa palikokuwa nyumbani
kwake kwake anaagwa.
Sista Kapuli anakwenda kupumzishwa/kulazwa/kuzikwa, na
anatuachia maswali mengi. Pengine maswali hayo hatuwezi kupata majibu yake sasa katika
wakati kama huu angekuwa anaweza kusema tungemuuliza maswali, tungemuuliza Sista Kapuli!
Ilikuwaje, bila shaka tungemuuliza na ninaamini asingekuwa najibu refu, asingekuwa
na jibu refu na ndilo jibu analotupa sasa.
Anasema kama Ayubu, “Laiti maneno
yangu yangeandikwa” akimaanisha yangebaki watu wasome, wajifunze. Laiti maneno yangu
yangeandikwa. Ayubu ni kati ya watu wa nyakati hizo za zamani alipita majaribu makubwa
ikiwemo kupoteza mali zake na kupata mateso makubwa ya kimwili, ya kiroho, ya kijamii
na hata ya kiakili.
Na katika mazingira yake wengi waliamini amelaaniwa na
Mungu na wakamshawishi amuache Mungu. Lakini yeye akasema “laiti maneno yangu yangendikwa”,
yangeandikwa ili yadumu, lakini basi hayajaandikwa, lakini anasema “najua wazi mkombozi
wangu anaishi”. Na huyu mkombozi wangu mwishowe atanipa haki yangu hapa duniani. (Ayubu
19:25).
Nafikiri Sista Kapuli angewaza kusema hivyo hivyo: “najua wazi mkombozi
wangu anaishi, mwili wangu umeharibiwa, uwezo wangu wa kuishi umeondolewa, lakini
pamoja na kuharibiwa mwili wangu huu, najua mkombozi wangu anaishi, atanipa haki yangu
hapa hapa duniani. Tutasema “atasemaje hivyo”? ni kweli bado tunaye na bado atalazwa
katika maeneo yetu/ ardhi yetu, kaburi lake litakuwepo nasi siku zote. Kwa hiyo ana
haki ya kusema atanipa haki yangu hapa hapa duniani. Yeye pekee angeweza kusema
ukali wa maumivu aliyopata, mateso aliyopata na angeweza kutuambia na nani aliyefanya
vile, lakini amebadilisha mwelekeo wake, hamtazami aliyetenda hicho, hamtazami aliyemtenda
hayo, anamtazama mkombozi wake; “Najua mkombozi wangu yu hai, atanipa haki yangu.
Kwa nini hamtazami aliyetenda hivyo? Kwa sababu anajua kuishi kwake na kufa kwake
ilikuwa kwa ajili ya Mungu, sio kwa ajili yake yeye mwenyewe.
Mtume Paulo
amewaambia Warumi, “ iwapo twaishi au tunakufa ni kwa ajili ya Mungu”. Kwa hiyo analielekeza
tumaini lake kwa mkombozi wake, “mkombozi wangu yu hai, na atanipa haki yangu na mwisho
nitamwona Mungu” Haya yatakuwa ni maneno yake Sista Crescentia alipofariki hayatuondolei
msiba, hayatuondolei uchungu tulio nao, lakini ni maneno yake ya kutupa sisi faraja,
ya kutujenga kiimani. Ningekuwa najua walihusika kwa namna moja au nyingine kwa
kifo cha Sista wako hapa, ningekuwa najua aliyekula njama hiyo au aliyemsaliti sista
kwa namna mojawapo basi ningewauliza, unapata faida gani kutoa uhai wa mwanadamu mwenzako
ili hali na wewe siku moja utakufa? Unapata fahari gani? Yawezekana amesukumwa na
tamaa fedha, yawezekana, kwamba, walifikiri sista ana fedha, au yawezekana kuna mtu
aliwatuma kwamba atawapa fedha, yawezekana, lakini fedha hizo zina raha gani, fedha
hizo za damu, fedha hizo zina raha gani, utapata faida gani?
Wanaweza kusema
maisha ni magumu lakini ugumu wa maisha unaondolewa kwa kumwaga damu?, ugumu wa maisha
unaisha kwa kuua? Unapomuua mwanadamu mwenzako ni sawa na unajiua mwenyewe. Hivi hivi
wahenga walisema “auae kwa upanga atakufa kwa upanga”. Maandiko yanasema “tamaa ikikua
inazaa dhambi na dhambi ikikua inazaa mauti”.
Uuaji huu una faida gani kwa
anayetenda. Hata hapa hatuwezi kupata jibu kwa sababu hawawezi kuwa na ujasiri wa
kutujibu au pengine hawako hapa au pengine hawajui kiswahili, inawezekana. Hakuna
faida kuua ili kupata unafuu. Hakuna faida wala hakuna raha kupata mali kwa kuangamiza.
Na wala kupata mali kwa kuangamiza hakuondoi ugumu wa maisha. Sana sana tunajenga
uasi na mwisho wa dhambi ni mauti vile vile.
Tukumbuke, tukumbuke tunaokuwa
na maelekeo ya kudhulumu uhai kwa sababu hizi za kimaisha. Tukumbuke, tukumbuke kila
anayeishi na anayekufa ni wake Mungu. Sisi sote ni wake Mungu tuwe tunaishi au tumekufa.
Tukumbuke kila wakati kwamba, Maandiko yanatumbia “sisi sote tutasimama mbele ya kiti
cha hukumu cha Mungu”.
Nafikiri pengine mtu ambaye amepungukiwa kabisa akili
hawezi kuelewa kwamba yeye ni kiumbe. Tukumbuke kwamba, sisi sote ni viumbe wa Mungu,
pamoja na tabia zetu mbaya, pamoja na mipango yetu mibaya, sisi sote ni viumbe wa
Mungu. Na mtume Paulo alipowaambia Warumi (14:10), anatuambia na sisi: “sisi sote
tutasimama mbele ya kiti cha hukumu ya Mungu”. Ndiyo maana Sista anasema “mtetezi
wangu yu hai, atanipa haki yangu”.
Mtume Paulo anasema “kila mtu atatoa habari
zake mwenyewe mbele yake”. Sasa ni ipi ingekuwa mbegu safi?, ni mbegu ya wokovu, ni
mbegu inayoita kwenye toba, ni mbegu inayoalika kwenye toba, inayoalika mageuzi. Kwamba,
kwa kutenda hivi, matokeo yake ni haya, mabaya hivi, yanayowafanya watu kwa maisha
yote wanasononeka, wanatokwa na machozi, kwa sababu tu ya mkono wangu, yanayowafanya
watu wanaacha shughuli zote nyingine na kubaki wanahangaika kwa sababu tu ya mkono
wangu, kwa sababu tu ya mipango yetu, kwa sababu tu ya kutamani hizo fedha, na hivyo
tumefanya kitendo ambacho kimeondoa uhai wa mwanadamu mwenzetu, na yeye alinyonya
kama sisi na anaishi kama sisi, ni kitu kibaya, ni mwaliko wa toba na wongofu na wa
mageuzi. Ni mwaliko unaoita mabadiliko.
Si tukio la pekee hili katika nchi
yetu. Yanatokea matukio kama haya. Lakini hatuwezi kuacha kutoa mwaliko huo, ndiyo
jibu pekee, kwamba, kwa kuuana hatuwezi kuondoa ugumu tunaouona maishani petu, kwa
kuuana hatuwezi kupata utajiri na ustawi tunaoutamani, kwa kuuana hatuwezi kutuliza
hasira yetu au chuki yetu tuliyo nayo. Tutaendelea kusema hivyo na hatuna njia nyingine.
Ni hili hasa linaloweza kutuhakikishia amani na utulivu tunaoutamani. Niliwahi
kusali na wafungwa mahali fulani. Waliniambia: “Baba tunaomba utupelekee salamu kwa
watanzania, uwambie kwamba, tumekosa. Pili tunaahidi kutokurudia na tatu watupe nafasi
tena tushuhudie kwamba, sisi pia tunaweza kuwa watu wema”. Na mmoja akaniambia: “tena
nikitoka nitakuwa mhubiri kuliko hata ninyi”.
Alikuwa anaongea maneno yanayomtoka
moyoni, lakini bado unasema, lakini mbona bado pamoja na hivi mnavyosema bado unasikia
kwingine mtu ametenda kitu kibaya kingine tena, pengine kibaya zaidi kuliko walichotenda
ninyi. Wale wote ambao tunafikiri tuna chuki, na chuki ambayo inaweza kusababisha
kifo cha mtu mwingine ni wakati wa kuongoka sasa. Tutaulizwa na Mungu. Sisi sote ni
mali yake Mungu na tutasimama mbele ya hukumu, mbele yake.
Ndugu zangu mliopo
hapa waombolezaji, jambo kubwa la kuwambieni, pole! Pole Mapadre, na kwa Baba Padre
Meneja wa miradi, Paroko, msaidizi wake, watawa, pole mkuu wa shule na timu yako,
poleni sana wanafunzi mliokuwa mnahudumiwa na Sista, poleni Shirika, waamini wote
wa Parokia hii, viongozi wetu wa serikali, wakuu wetu wa usalama, raia wa Tanzania,
Poleni kwa msiba huu unaotupa aibu, unaotupa aibu na uchungu mkubwa. Poleni!
Njia
za uovu zinakuwepo katika jamii, tusikate tamaa, wanafunzi msikate tamaa, walimu na
walezi msikate tamaa, watawa msikate tamaa. Endeleeni kuwa na njaa na kiu ya haki
kwani hiyo ni njaa na kiu ya kutamani kutenda anayotaka Mungu. Hiyo ndiyo hekima,
endeleeni kuwa na njaa na kiu ya haki. Jambo ambalo analifahamu mtu kuwa ni la kweli
hawezi kulikana kwa hiyo msianze kukana yaliyo ya kweli. Mtakatifu Karoli Lwanga alisema:
“analofahamu mtu kuwa ni la kweli hawezi kulikana”. Na ninyi vilevile mnalojua kuwa
ni la kweli msilikane. Yawezekana tukapatwa mateso mengi zaidi, yawezekana tukapata
hasara kubwa zaidi, lakini tukiishi au tunakufa tukumbuke tupo kwa ajili ya mapenzi
ya Mungu. Msiogope!, msiogope! Kuweni watu wa rehema, samehe tu, samehe tu, kama Mungu
angewasukuma wakaomba msamaha tungefurahi, tungegeuka na kusema Mungu mkubwa, lakini
Shetani anapenda pia kuwa na raia wake, kwa hivyo hawezi kusema Mungu mkubwa, hivyo
muwasamehe tu ..........AMINA. Imeandaliwa na Padre Joseph Peter Mosha,