2014-06-27 08:04:55

Mgonjwa kwanza, mengine baadaye!


Bwana Maurizio Guizzardi mkurugenzi mkuu wa Hospitali ya Agostino Gemelli iliyoko mjini Roma katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Kitivo cha tiba na upasuaji cha Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu, anasema, wagonjwa wengi kutoka ndani na nje ya Italiwa wameendelea kupata huduma ya kinga na tiba kwa kutumia teknolojia na utaalam wa kisasa kabisa katika kuwahudumia wagonjwa kwa kuzingatia mahitaji yao msingi: kiroho na kimwili.

Hospitali imekuwa ikiwahudumia wagonjwa na ndugu zao katika mazingira ya upendo na mshikamano wa dhati kwa kutambua kwamba, Kitivo hiki ni kati ya vitivo vinavyoongoza nchini Italia katika huduma za kinga na tiba pamoja na tafiti za kisayansi. Hapa wanafundwa kitaaluma waganga, wauguzu na wafanyakazi katika sekta ya afya katika ujumla wake.

Ni hospitali ambayo inaongoza katika mkoa wa Lazio kuwa kulaza na kuwahudumia wagonjwa wengi. Ni hospitali kubwa kitaifa inayotibu ugonjwa wa saratani na kwamba, hapa ni kimbilio kwa magonjwa yaliyoshindikana sehemu mbali mbali za mkoa wa Lazio.

Bwana Guizzardi anasema, athari za myumbo wa uchumi kimataifa hazipaswi kamwe kuathiri tija na huduma inayotolewa hospitalini hapo na kwamba, hospitali itaendelea kuwafunda wafanyakazi wake, ili waweze kutoa huduma bora zaidi kwa wagonjwa na jamaa zao.

Professa Franco Anelli, mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu anasema, miaka 50 iliyopita, ulikuwa ni mwanzo wa historia ya Chuo kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu, kwa kuwaonjesha watu furaha wakati wa uzinduzi wake, simanzi na uchungu wakati watu wanapolazwa, lakini daima watu wameendelea kuonesha matumaini kutokana na huduma bora ya kinga na tiba inayotolewa hospitalini hapo, kwa kumpatia mgonjwa kipaumbele cha kwanza.

Wafanyakazi hospitalini hapo ni watu wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya huduma kwa wagonjwa. Hapa sayansi na imani vinakamilishana, kiasi kwamba, Chuo kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu, kimeendelea kuwa aminifu kwa mwongozo wa muasisi wake Padre Agostino Gemelli. Chuo kimeendelea kusoma alama za nyakati ili kuhakikisha kwamba, kinatoa huduma makini kwa kuzingatia tafiti za kisayansi na teknlojia iliyoko uwanjani. Hapa ni mahali pa kukinga na kutibu maradhi; majiundo makini na tafiti za kisayansi.

Professa Rocco Bellantone, Mkuu wa kitivo cha tiba na upasuaji cha Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu anasema, kila siku wako bega kwa bega na wagonjwa wanaosumbuka na kuteseka kama sehemu maalum ya utume wao.

Wamejifunza kwamba, wao wanapaswa kujisadaka kwa ajili ya kumhudumia binadamu mzima: kiroho na kimwili. Wagonjwa wanapewa dawa na kuonjeshwa upendo wa dhati unaojikita katika huduma makini. Katika shida na mahangaiko, wagonjwa wanapaswa kuoneshwa mwanga wa imani kutoka kwa Mwenyezi Mungu anayeponya na kufariji.

Kutokana na changamoto hii, wahudumu wa sekta ya afya wataendelea kuchakarika ili kuhakikisha kwamba, wanamhudumia mgonjwa kikamilifu na kamwe hawawezi kuridhika na kiwango cha huduma wanachokitoa kwa sasa. Kila siku katika waganga na watafiti wanajikuta wakikabiliana na changamoto mbali mbali kutoka kwa wagonjwa, changamoto ambazo zinapaswa kufanyiwa kazi kwa ujasiri pasi na kukata tamaa.

Katika kipindi cha kuanzia mwaka 1961 hadi mwaka 1964 Gemelli ikawa ni Hospitali kubwa inayotegemewa na wengi. Ni hsopitali ambayo ni jukwaa la Chuo kikuu cha Kikatoliki. Hapa si mahali pa kujifunza peke yake, kwani mganga anaishi kwa ajili ya kumhudumia mgonjwa. Hospitalini hapa mgonjwa anaheshimiwa na kuthaminiwa kwa kuzingatia kanuni za ukweli, umakini na huruma.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.