2014-06-27 07:51:16

Majanga ya Boko Haram


Askofu mkuu Ignatius Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria anasema kwamba, vitendo vya kigaidi vinavyoendeshwa na Kikundi cha Boko Haram vina madhara makubwa kwa maisha ya watu na mali zao. RealAudioMP3

Ni matumaini ya Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria kwamba, wasichana waliotekwa nyara wataweza kuachiliwa huru mara moja na kwamba, kuna haja kwa Serikali ya Nigeria kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru wa kuabudu, haki, amani na usalama wa wananchi wake.

Askofu mkuu Kaigama ameyasema hayo hivi karibuni katika Kongamano la Kimataifa lililoandaliwa na Shirika la Kipapa linalosaidia Makanisa hitaji kuhusu uhuru wa kidini, huko nchini Malta. Hivi karibuni, wasichana wa shule 276 walitekwa nyara na kikundi cha Boko Haram, kati yao 53 ndio waliofanikiwa kuwatoroka watesi wao. Wasichana hawa ni waamini wa dini mbali mbali nchini Nigeria, kumbe, lengo si kwa ajili ya kuwasilimisha Wakristo tu, bali kuhakikisha kwamba, Nigeria inatawaliwa na “Sharia” za dini ya Kiislam.

Boko Haram inataka kusambaratisha tunu msingi za maisha ya Kikristo nchini Nigeria kwa madai kwamba, zinataka kurithisha utamaduni kutoka nchi za Magharibi ambazo kadiri ya Boko Haram ni tamaduni harem. Hili ni jambo ambalo linakwenda kinyume kabisa na haki msingi za binadamu pamoja na uhuru wa kuabudu. Watu wanapaswa kuheshimiana na kuthaminiana hata katika tofauti zao kwani tofauti hizi si kwa bahati mbaya bali ni mpango wa Mungu, ili watu waweze kutajirishana.

Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria linabaianisha kwamba, tangu mwaka 2009 Boko Haram ilipoanza kufanya mashambulizi ya kigaidi nchini Nigeria, watu wengi wamepoteza maisha na mali pamoja na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundo mbinu. Vitendo vya kigaidi vinavyoendeshwa na Boko Haram vimewafanya wananchi wengi wa Nigeria kukosa imani na Serikali, kwani imeonesha udhaifu mkubwa katika kudhibiti vitendo vya kigaidi nchini humo.

Jambo hili linaonesha kwamba, pengine kuna baadhi ya viongozi wa Serikali na wanasiasa wanatetea masilahi binafsi, lakini wakumbuke kwamba, watu wanaendelea kupoteza maisha na mali zao. Rasilimali fedha na watu iliyotengwa kupambana na Boko Haram imetumika vibra kutokana na kukithiri kwa tabia ya rushwa na ufisadi nchini Nigeria.

Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuisaidia Nigeria kupambana na Boko Haram kwa kufanya upembuzi yakinifu wa mahali ambapo Boko Haram wanapata silaha za moto ambazo zimekuwa ni tishio kwa usalama na maisha ya wananchi wa Nigeria. Ni haki na vyema kuwafahamu watu wanaofadhili vitendo vya kigaidi nchini Nigeria ili waweze kushughulikiwa kikamilifu na Jumuiya ya Kimataifa, kwani ni jambo la kusikitisha kuona kwamba, kuna watu wanaotaka kupata utajiri wa haraka haraka kwa kumwaga damu ya watu wasiokuwa na hatia.

Kumbe, operesheni ya kijeshi iliyoanzishwa na Serikali bado haijafua dafu kwa Boko Haram. Ni vyema ikiwa kama Serikali itaibua mbinu mkakati wa kupambana na umaskini, ukosefu wa fursa za ajira pamoja na rushwa kwani haya ni mambo ambayo yanaendelea kuchochea vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na Boko Haram.








All the contents on this site are copyrighted ©.