2014-06-23 08:46:56

Jisadakeni kwa ajili ya jirani zenu!


Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo. Kisha kuadhimisha Sherehe ya Utatu Mtakatifu, ambamo tulimtukuza na kumshangilia Mungu katika Utatu, sasa tumeadhimisha sherehe ya Mwili na Damu ya Kristo, tunamshangilia Kristo aliye kifungo cha Upendo na Ishara ya Umoja. RealAudioMP3

Kristo Yesu amependa kukaa kwetu katika Sakramenti Takatifu sana ya EKaristi. Neno linasema “nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Kunyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi” Mt. 26:26-28.

Na pengine amesema “ Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo” Yoh. 14:1-3.

Kristo Yesu alipokuwa akiwaaga wanafunzi wake kabla ya kupaa kwake, aliahidi kurudi ili awakaribishe kwake. Kristo Yesu ametimiza neno hilo kwa uwepo wake katika Neno na Sakramenti. Kristo yupo nasi katika Neno lake, yupo nasi katika Sakramenti zake. Zaidi sana, yupo nasi katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu. Mafundisho ya imani yetu yanasema hivi: katika Sakramenti nyinginezo zote, tunapokea neema za Kristo ili zitusaidie kupata wokovu. Tunapokea nguvu ya Kristo. Lakini katika Sakramenti Takatifu sana ya Ekaristi, tunampokea Kristo Yesu mwenyewe katika mwili wake na damu yake, katika Umungu wake na Ubinadamu wake.

Kuanzia nyakati za Kanisa la mwanzo kabisa, kumekuwa na maadhimisho ya Karamu hii kuu, kwa ukumbusho wa Bwana kama alivyoagiza mwenyewe. Kadiri nyakati zilivyokwenda na uelewa wa mafumbo ya Kristo ulivyokuwa, Ibada rasmi zilianza kuwekwa, ikiwa ni pamoja na maandamano, ili kuweza kushuhudia hadharani Imani yetu kwa Yesu wa Ekaristi, huku tukikiri kuwa yeye ndiye mfalme wa maisha yetu, ni mwalimu wetu na kiongozi wetu, yupo kati yetu akituongoza kwenda kwa Baba.

Mashangilio ya sherehe hii, tulipaswa kuyafanya siku ya Alhamisi kuu. Lakini kwa sababu za kichungaji, kwamba hatuwezi kufanya mashangilio mazito kipindi kile cha Kwaresma, ili kutuacha tutafakari kwa kina zaidi fumbo la mateso ya Kristo, Mama Kanisa ametuwekea siku maalumu baada ya Sherehe ya Utatu Mtakatifu, tuweze kusherehekea hadharani na kukiri imani yetu kwa Yesu wa Ekaristi waziwazi.

Kwa nini tunaandamana na Kristo Yesu wa Ekaristi kwa mashangilio makubwa hivi? Maana yake ni hii: Sisi hapa duniani ni Kanisa linalosafiri, Kanisa linalohiji. Na katika safari yetu hii, kuna mawimbi na mitikisiko mbalimbali ambayo huweza kukwamisha kabisa safari yetu ya kwenda kwa Baba. Tunaandamana tukiwa na Yesu wa Ekaristi tukiwa tunaungama kwamba, safari yetu hii ya kwenda kwa Baba, itakuwa salama endapo tu, tutakuwa tayari kuwa na Yesu, kuwa tayari kuongozwa na Neno lake, kuwa tayari kurutubishwa na Sakramenti zake.

Hivyo, yale maandamano ya Sherehe ya Mwili na Damu ya Kristo, ndiyo muhutasari wa maisha binafsi mwamini. Swali ambatanishi hapa ni hili: katika safari ya maisha yako unaongozwa na nini? Nani anayaongoza maisha yako? Dira yako haswa ni nni? Na lengo la safari yako ni nini? Hapo tunaalikwa kutafakari kwa uzito zaidi juu ya uwepo wa Kristo Yesu katika maisha yetu ya kila siku.

Tukiligeukia Kanisa la nyumbani, yaani familia tutashududia kwamba, familia zetu kama Kanisa dogo la nyumbani linapata mitikisiko mibaya mno, inayowapelekea wanafamilia kukata tamaa ya kendelea kusafiri pamoja kuelekea ukamilifu. Na hakuna anayefurahia mitikisiko hiyo. Dawa ni nini? Ni Yesu wa Ekaristi, tumpokee katika Neno lake, neno lake lituongoze, tumpokee katika Sakramenti zake, akae katika mioyo yetu, akae katika familia zetu, awe nasi maishani mwetu mwote.

Katika famili zetu, tusipokuwa tayari kumwinua Yesu na kuongozwa naye katika upendo wake, katika unyenyekevu wake, katika huruma yake, katika msamaha wake, katika uvumilivu wake, katika haki yake na katika imani yake, hapo hatuwezi kuwa salama. Wengi wetu badala ya kumwinua Yesu na kuambatana naye, tunaambatana na tamaa za mali na mafanikio, tunaambatana na mioyo inayotamani vita, tunainua juu tabia zetu mbaya, tunainua ngumi na kelele za matusi badala ya kumwinua Yesu, na hapo ndipo unapozuka moto wa fujo ndani ya familia, hadi kupelekea safari ya pamoja kuvunjika.

Sherehe hii na mashangilio yake vinatukumbusha sote tuwe watu wa Kiekaristi. Familia zetu ziwe za Kiekaristi, parokia zetu ziwe za Kiekaristi, Majimbo yetu yawe ya Kiekaristi. Tukubali sote kuongozwa na Yesu wa Ekaristi, Mungu wa upendo na Mfalme wa amani anayetuongoza katika safari yetu hii ya kumwendea Mungu.

Mwisho tutoe rai ya kichungaji kwetu sote tunaoliungama jina la Kristo Yesu ndani ya Kanisa Takatifu. Kila mmoja afanye jitihada kubwa ya akili, mwili na roho ili kulinda imani na heshima kuu kwa Sakramenti takatifu sana ya Ekaristi. Nguzo mbili muhimu sana kwa imani yetu ni NENO la MUNGU na Sakramenti Takatifu sana ya Ekaristi. Tukijiruhusu kuchezacheza na Neno la Mungu, au kuchezacheza na Ekaristi Takatifu, hapo tunacheza na misingi, hatutabaki salama. Tuungane pamoja na makuhani wetu, kudhibiti kabisa hila zote na kufuru zinazotendwa dhidi ya Sakramenti Takatifu sana.

Nasi sote, tupende kumpokea Kristo Yesu katika Sakramenti ya Mwili na damu yake, katika hali njema ili tupate uzima tulioahidiwa. Lakini pia tukwepe kabisa tabia ya kumpokea pasipo kustahili: mwenyewe alisema, tukifanya hivyo, tunakula hukumu. Hatupati amani, faraja na kitulizo rohoni, wala uzima endapo tunampokea katika hali ya kufuru.

Pamoja na hayo, tunaalika na kuhimiza sana, tupende kuiabudu Sakramenti ya Ekaristi takatifu. Tuketi miguuni pake, tumwage mioyo yetu mbele yake, tumpatie furaha zetu na uchungu wetu, tumpe mipango ya maisha yetu aibariki, tumpe pia mapungufu na kushindwa kwetu ili atuinue, tumpe marafiki zetu na wapendwa wetu awabariki, tumpe pia maadui zetu na watesi wetu awaguse kwa neema zake, tumtegee sikio la moyo, tulisikie neno lake katika ukimya mtakatifu, naye yupo tayari anatungoja, atusikilize. Yesu ni rafiki wa pekee asiyechoka kutusikiliza.

Ibada kwa Ekaristi Takatifu ni kiini cha Ibada zote katika Kanisa. Ibada nyingine zote zinatuelekeza kwa Yesu. Ibada kwa Yesu wa Ekatisti inatupatia muungano kamili naye mwenyewe aliye njia, ukweli na uzima. Tenga walao nusu saa tu katika wiki, ukamwabudu Yesu wa Ekaristi, ukishazoea utaweza kufanya zaidi, na utaonja heri ya kuwa karibu na Yesu, na usikose kuwaalika wengine kwenda kwa Yesu.

Kutoka studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.







All the contents on this site are copyrighted ©.