2014-06-21 12:44:43

Balozi wa Vatican nchini Sudan ya Kusini awasilisha hati za utambulisho!


Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya na Sudan ya Kusini, hivi karibuni aliwasilisha hati zake za utambulisho kwa Rais Salva Kiir wa Sudan ya Kusini, alipotembelea hivi karibuni Jimbo kuu la Juba.

Askofu mkuu Balvo anasema, Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kufuatilia kwa karibu zaidi matukio mbali mbali yanayotendeka nchini Sudan ya Kusini, hasa kutokana na mahangaiko ya watu wasiokuwa na hatia; mambo ambayo yanasababishwa na machafuko ya kisiasa nchini Sudan ya Kusini.

Askofu mkuu Balvo anaendelea kuwahimiza wadau wakuu wa mkataba wa amani nchini Sudan ya Kusini, kuhakikisha kwamba, wanatekeleza dhamana hii nyeti kwa ajili ya kulinda na kudumisha amani na utulivu Sudan ya Kusini; mambo msingi katika kukoleza maendeleo endelevu ya binadamu. Upatikanaji wa amani ya kudumu nchini Sudan ya Kusini utawasaidia wananchi kurudi tena kwenye makazi yao na kuendelea na shughuli za kilimo na uzalishaji mali.

Askofu mkuu Balvo amelitaka Kanisa pia kuendelea kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kudumisha misingi ya haki, amani, umoja, mshikamano, majadiliano na upatanisho wa kitaifa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Sudan ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.