2014-06-20 10:22:24

Wakimbizi na changamoto zao!


Jumuiya ya Kimataifa tarehe 20 Juni inaadhimisha Siku ya Wakimbizi Duniani. Takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni 45 wanaolazimika kuzikimbia nchi zao ili kutafuta maisha bora zaidi ugenini. Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Barani Ulaya, Caritas Europe linasema kwamba, kuna maelfu ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaoingia Barani Ulaya kwa njia ya Bahari.

Hawa ni watu wanaotafuta kimsingi: amani, utulivu, demokrasia, utu na maendeleo yao. Hii ni changamoto kwa Nchi za Ulaya kuhakikisha kwamba, zinatengeneza sera na mikakati inayojikita katika ukarimu, udhibiti na ushirikishwaji katika kuwapokea na kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji wanaowasili kila siku Barani Ulaya. Nchi za Ulaya ziweke sheria ambazo zitawawezesha watu kuhamia kihalali, kuliko mtindo wa sasa wa kuwa na kundi kubwa la wahamiaji haramu.

Wahamiaji wanaotafuta fursa za ajira wapewe vibali; wale wanaokimbia vita na majanga asilia wapokelewe kwa heshima na kwamba, vibali viwasaidie wahamiaji hawa kuwa na uhuru wa kutembea. Kuna kundi kubwa la wahamiaji linalihifadhiwa nchini Italia.

Caritas inatambua ukarimu, lakini pia inakiri shida na magumu wanayokabiliana nayo wahamiaji hawa huko kambini. Ili kukabiliana na changamoto hii kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kusaidiana kwa hali na mali, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Siku ya Wakimbizi Duniani kwa Mwaka 2014.







All the contents on this site are copyrighted ©.