2014-06-20 14:01:10

Ukosefu wa uhuru wa kidini unahatarisha amani, maendeleo na mshikamano wa watu!


Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanaonesha utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Historia ya Kanisa kwa kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru wa kidini, kwa kutambua kwamba, kil mtu ni muasisi wa ukweli kuhusu asili na hatima ya maisha yake. Ndani mwake kuna maswali na mawazo ambayo kamwe hayawezi kuchakachuliwa kwa vile yanapata chimbuko lake kutoka katika undani wa utu wake mwenyewe.

Haya ni masuala ya kidini na uhuru wa kuabudu yanayojitokeza daima katika maisha ya mwanadamu, kwa kuonesha umuhimu wake, uhusiano na ulimwengu, historia na kuondoa giza linaloyasakama maisha ya binadamu, kwani mwanadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko Ijumaa tarehe 20 Juni 2014 wakati alipokuwa anazungumza na wajumbe wa kongamano la kimataifa lililokuwa linafanyika kwenye Chuo Kikuu cha LUMSA kilichoko mjini Roma kuhusu "uhuru wa kidini mintarafu sheria za kimataifa pamoja na kinzani za tunu msingi za maisha".

Uhuru wa kidini ni haki msingi inayoonesha utu unaomsukuma mwanadamu kutafuta ukweli na kuukumbatia kwa kutambua nguvu iliyomo ndani mwake inayoweza kumsaidia kutumia uwezo wake wote. Uhuru wa kidini ni mchakato unaomwezesha mtu kuishi mintarafu kanuni msingi za kimaadili zinazobubujika kutokana na ukweli uliopatikana katika maisha binafsi au katika hadhara.

Uhuru wa kidini ni kati ya changamoto kubwa katika ulimwengu wa utandawazi ambamo mawazo dhaifu yanaonekana kutawala zaidi kwa kisingizio cha maridhiano, hali ambayo wakati mwingine inapelekea madhulumu kwa wale wanaosimama kidete kulinda na kumtetea mwanadamu na kanuni maadili.

Sheria za kimataifa na kitaifa zinapaswa kutambua na kutetea uhuru wa kidini ambao kimsingi ni sehemu ya utu wa binadamu inayomwezesha kuwa kweli huru na kwamba, hiki ni kiashiria cha demokrasia na kanuni msingi ya uwepo wa Serikali yoyote ile! Uhuru wa kidini ukitambuliwa na kusimamiwa kikamilifu ni chachu ya maendeleo na mahusiano bora katika jamii, serikali na dini mbali mbali. Hapa dini na serikali zinaweza kushirikiana kwa dhati bila ya kuingiliana katika majukumu yake.

Mmong'onyoko wa tunu msingi za kimaadili unaweza kudhibitiwa kwa kuzingatia kanuni msingi zinazokubalika na wengi, ili kudumisha mshikamano kwa ajili ya mafao ya wengi. Lakini ukweli wa mambo unaonesha kwamba, leo hii bado kuna udhibiti mkubwa wa haki msingi za binadamu na ubaguzi unaotokana na mwelekeo wa imani ya mtu, kiasi kwamba, hata wakati mwingine, kumekuwepo na madhulumu na nyanyaso za wazi kabisa, mambo yanayochafua akili, amani na hatimaye kunyanyasa utu wa binadamu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, kwa bahati mbaya Wakristo sehemu mbali mbali za dunia ndilo kundi ambalo limeendelea kunyanyaswa, kudhulumiwa na kutengwa, hali ambayo kwa nyakati hizi inaonekana kuongezeka maradufu kuliko hata ilivyokuwa kwa Kanisa la Mwanzo, tangu wakati ule Costantino alipochapisha Waraka wa uhuru wa kidini kwa Wakristo.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, kongamano hili litasaidia kupambanua hoja za kisayansi na sababu zinazotaka sheria kuheshimu na kulinda uhuru wa kidini.







All the contents on this site are copyrighted ©.