Mshikamano wa upendo na wahamiaji kutoka Kaskazini mwa Afrika!
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika ya Kaskazini, CERNA katika mkutano
wake wa mwaka uliofanyika mjini Roma hivi karibuni linasema kwamba, litaendelea kusimama
kidete kuwalinda, kuwatetea na kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji kutoka Kaskazini
mwa Afrika, lakini kamwe halitasita kukemea nyanyaso na dhuluma wanazotendewa wakimbizi
na wahamiaji hawa sehemu mbali mbali za dunia.
Maaskofu katika mkutano wao
wamejadili pamoja na mambo mengine ujasiri, matumaini na imani inayoshuhudiwa na wakimbizi
pamoja na wahamiaji katika Jumuiya zile ambazo wanapokelewa kwa heshima na tahadhima,
kiasi kwamba wanakuwa ni chachu ya maisha mapya. Maaskofu wanasikitishwa na mambo
ambayo yanapelekea kwa wananchi wengi kutoka Kaskazini mwa Afrika kuzikimbia nchi
zao, ili kutafuta nafuuu ya maisha ughaibuni ambako wengi wao wanateseka sana.
Kuna
baadhi ya watu ambao wananyanyaswa, utu na heshima yao havithaminiwi, kiasi cha kujikuta
wanatumbukia katika biashara haramu ya binadamu au kuchukuliwa kuwa wahuni na watu
wasiotakikana katika jamii, kumbe kimsingi ni watu waliokuwa na heshima zao huko wanako
toka! Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kulihamasisha Kanisa na watu wenye mapenzi
mema kuwa makini dhidi ya biashara haramu ya binadamu inayoendelea kunyanyasa utu
na heshima ya binadamu sehemu mbali mbali za dunia. Kuna wanawake na watoto ambao
wametumbukizwa katika utumwa mamboleo.
Wakimbizi na wahamiaji wanaofika Kaskazini
kwa Afrika kutoka Kusini mwa Jangwa la Sahara wanapaswa kupokelewa na kutunzwa kwa
heshima na wala wasifikiriwe kwamba ni "wageni wa kuja na kupita" kama ilivyobainishwa
huko Morocco. Hapa kuna haja ya kuwa na mikakati makini ya kuwapokea na kuwahudumia
wahamiaji na wakimbizi katika mahitaji yao msingi: kiroho na kimwili. Maaskofu kutoka
Afrika ya Kaskazini wanawashukuru wale wote wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya kuwahudumia
wakimbizi na wahamiaji kutoka Barani Afrika pamoja na kusaidia mchakato wa taasisi
zinazowapokea kuzingatia sheria za kimataifa pamoja na haki msingi za binadamu.
Shirikisho
la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kaskazini mwa Afrika limepembua pia hali halisi ya
kisiasa, kijamii na kiuchumi inayoendelea kujitokeza katika Nchi za Afrika ya Kaskazini
na athari zake katika maisha, ustawi na maendeleo ya wengi. Maaskofu wanasema, kumekuwepo
na mfumuko mkubwa wa familia kutengana kutokana na vishawishi vya maendeleo na mambo
ya ulimwengu, jambo ambalo linatishia ustawi na mshikamano wa kifamilia.
Kuna
idadi kubwa ya wanafunzi wanaotoka Kusini mwa Jangwa la Sahara wanaotafuta nafasi
za masomo na majiundo makini Kaskazini mwa Afrika, jambo ambalo linahitaji kweli kuwa
na mshikamano wa mikakati na shughuli za kichungaji kimataifa, ili kuwasaidia wanafunzi
hawa kufikia lengo lao msingi, yaani kupata elimu, ujuzi na maarifa, vinginevyo wanaweza
kujikuta wametumbukia kwenye genge la walanguzi na wahuni. Hii ni changamoto kwa wadau
mbali mbali kutoa taswira kamili ya Kanisa la Kristo Kaskazini mwa Afrika.
Kutokana
na changamoto hiz, CERNA inaandaa Waraka wa pamoja utakuwa kugusia kuhusu wajibu wao
wa kuwa ni wahudumu wa fadhila ya matumaini na kwamba, wanatarajia kuiwasilisha kwa
Baba Mtakatifu ifikapo mwaka 2015, wakati wakatapokuwa wanafanya hija yao ya kitume
inayofanyika kila baada ya miaka mitano mjini Vatican. Maaskofu wakati wa mkutano
wao hapa mjini Roma, wamebahatika pia kushiriki katika Ibada za Misa Takatifu zilizokuwa
zinaendeshwa na Baba Mtakatifu, wakashuhudia unyenyekevu na changamoto zake kwa ajili
ya maisha na utume wa Kanisa la Kristo.
Maaskofu kutoka Kaskazini mwa Afrika
wameangalia pia kuhusu maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu Familia yatakayoanza
kutimua vumbi mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba, 2014. Waamini
wengi kutoka Kaskazini mwa Afrika wanaishi katika ndoa mseto, changamoto ya kutafuta
mbinu na mikakati ya kuziwezesha familia hizi kuendelea kutekeleza dhamana na wajibu
wake wa malezi na majiundo kwa watoto wao.
Maaskofu wamekazia pia umuhimu wa
kuendeleza majadiliano ya kidini na kiekumene Kaskazini mwa Afrika, kwa kutambua kwamba
hii ni changamoto kubwa na kadiri inavyokuwa ngumu hivyo ndivyo inavyowawajibisha
kuendelea kusonga mbele kwa imani na matumaini pasi na kukata tamaa. Kuna haja pia
ya kuratibu shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na wakimbizi kutoka sehemu mbali
mbali za Bara la Afrika kwa kushirikiana na wadau wengine kwani hii ni dhamana nyeti,
peke yao inaweza kuwaelemea na hivyo kushindwa kuitekeleza barabara.
Shirikisho
la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kaskazini mwa Afrika, limeonesha wasi wasi wake kutokana
na ghasia pamoja na kinzani za kijamii zinazoendelea kujitokeza nchini Lybia, kiasi
kwamba, baadhi ya viongozi wa Kanisa kutoka Lybia wameshindwa kutoka nchini humo kwa
sababu za kiusalama. Mkutano wa CERNA utafanyika tena hapo tarehe 8 Mei 2015 mjini
Roma wakati wa hija za kitume mjini Vatican. Itakumbukwa kwamba, CERNA inaunganisha
nchi za Algeria, Lybia, Tunisia na Morocco.