2014-06-19 10:20:04

Ukabila na udini hauna mashiko tena!


Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya amewataka wananchi wote wa Kenya kushikamana kwa pamoja ili kujenga na kudumisha umoja na mshikamano wa kitaifa, ili kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho na kwamba, sera za kikabila na kidini zinazotaka kuwagawa wananchi wa Kenya hazina mashiko wala ustawi kwa maendeleo ya wananchi wa Kenya.

Ni dhamana na wajibu wa viongozi wa kisiasa nchini Kenya kuonesha ukomavu wao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora unaoshuhudiwa kwa njia ya maisha na maneno yao wanapokuwa jukwaani. Kila mtu anapaswa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kwa njia hii wananchi wa Kenya wanaweza kujenga mazingira ya kuheshimiana na kuthaminiana kama ndugu.

Kardinali John Njue ameyasema haya hivi karibuni wakati alipokuwa anatoa tuzo kwa wanamichezo bora walioshiriki katika michezo kwa ajili ya kukusanya fedha ili kusaidia mchakato wa kumtangaza Mtumishi wa Mungu Kardinali Maurice Otunga kuwa Mwenyeheri na hatimaye, Mtakatifu kadiri ya mapenzi ya Mungu. Mchakato kwa ngazi ya Kijimbo, ulioanza Novemba 2011 ulikamilika mwaka 2013 na sasa umepelekwa mjini Vatican kwa tathmini ya kina.

Ni matumaini ya Kardinali John Njue kwamba, Mtumishi wa Mungu Kardinali Otunga atakuwa ni Mkenya wa kwanza kuandikwa katika Orodha ya Watakatifu ndani ya Kanisa Katoliki.







All the contents on this site are copyrighted ©.