Miaka 10 ya Chuo Kikuu cha Mtakatifu Thoma wa Akwino!
Chuo Kikuu cha Mtakatifu Thoma wa Akwino, Burkina Faso chenye wanafunzi 1850 wanaopata
majiundo yao kwenye vitivo kumi, kinaadhimisha Miaka 10 tangu kilipoanzishwa. Hiki
ni chuo ambacho kimeendelea kupokea wanafunzi kutoka ndani na nje ya Burkina Faso
na kinasimamiwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Burkina Faso.
Maaskofu wanasema,
Chuo kikuu cha Mtakatifu Thoma wa Akwino, hakina budi kuwajengea wanafunzi wake utamaduni
wa kuwa waaminifu, waadilifu, wachapakazi, daima wakitafuta mafao ya wengi, ili kuweza
kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi
na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Kitivo cha Tiba cha Chuo Kikuu cha Mtakatifu
Thoma wa Akwino, hapo tarehe 28 Juni kitatoa shahada kwa Madaktari wake wa kwanza
kufuzu mafunzo chuoni hapo. Hawa ni Madaktari 24 watakaopata shahada ya kwanza na
kwamba, kwa sasa kuna mipango ya kuendelea kutoa elimu ya juu, ili kukidhi mahitaji
ya wataalam na mabingwa katika tiba ya mwanadamu.