2014-06-18 14:09:19

Waonjesheni wakimbizi, huruma na upendo!


Baba Mtakatifu mara baada ya Katekesi yake kuhusu Kanisa, amewakumbusha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwamba, tarehe 20 Juni 2014, Jumuiya ya Kimataifa itaadhimisha Siku ya Wakimbizi Duniani kwa Mwaka 2014. Hawa ni watu ambao wanalazimika kuzikimbia nchi zao kutokana na kinzani pamoja na madhulumu.

Idadi ya wakimbizi duniani inaendelea kuongezeka maradufu katika siku za hivi karibuni na kuna idadi kubwa ya watu wanaotamani kuzikimbia nchi zao ili kusalimisha maisha yao! Kuna mamillioni ya wakimbizi kutoka nchi na dini mbali mbali duniani wanaoishi katika majanga na madonda makubwa ya kijamii ambayo pengine itakuwa vigumu sana kuweza kuponywa.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuonesha moyo wa upendo na ukarimu kwa wakimbizi, kwa kushirikishana nao hofu na wasi wasi wa maisha yao kwa siku za usoni na pale inapowezekana kuwasaidia katika mahangaiko yao.

Baba Mtakatifu anawaombea watu na taasisi ambazo zinaendelea kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuonesha ukarimu na usalama, kwa kuwapokea na kuwatunza wakimbizi, huku wakizingatia utu na heshima yao, kama sehemu ya mchakato unaolenga kuwapatia matumaini.







All the contents on this site are copyrighted ©.