2014-06-17 08:28:03

Uwekezaji makini usaidie kuleta mabadiliko ya kweli katika Jamii!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 16 Juni 2014 amewashukuru na kuwapongeza wajumbe wanaohudhuria kongamano la kimataifa linalojadili kwa kina na mapana jinsi ya kuwekeza ili kuwajengea uwezo maskini katika kukabiliana na mazingira yao sanjari na kuondokana na ukosefu wa usawa na migawanyiko mikali ya kijamii, kiasi cha kundi kubwa la watu kuendelea kuogelea katika hali mbaya ya kijamii.

Mwekezaji makini ni mtu anayetumia rasilimali yake kwa ajili ya kukoleza maendeleo ya maskini kiuchumi na kijamii, ili kujikwamua kutoka katika mahitaji yao msingi yanayofumbatwa katika kilimo, maji safi na salama, makazi bora, huduma za elimu na afya. Uwekezaji wa namna hii unapania kuleta mabadiliko ya kweli katika maisha ya watu, kwa kutengeneza fursa za ajira, kuwapatia watu nafasi ya kupata huduma ya nishati, elimu pamoja na kuendeleza mchakato wa maboresho ya tija na uzalishaji katika sekta ya kilimo.

Matokeo ya uwekezaji makini yanapimwa kwa mchango wake. Lengo ni kujenga uhusiano wa dhati kati faida na mshikamano, uwekezaji unaolenga katika majitoleo na maboresho ya maisha ya watu. Ulimwengu mamboleo una kiu ya kutambua na kuthamini ukweli huu.

Baba Mtakatifu anasema, sekta ya uchumi na fedha haina budi kuratibiwa na kanuni maadili na kwamba, soko liwe ni kwa ajili ya huduma ya watu na mafao ya binadamu wote. Ni jambo lisilovumilika tena kuona kwamba, baadhi ya taasisi za fedha zinaendelea kujitajirisha badala ya kuhudumia watu katika mahitaji yao msingu au wachache wanaendelea kutajirika wakati mamillioni ya watu yanatumbukia katika janga la umaskini.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia yanaharakisha mzunguko wa fedha, kumbe kuna haja pia kuboresha uwezo wa kutoa huduma na kusimamia mafao ya wengi. Upandishaji wa bei ya mazao ya chakula ni kashfa kubwa inayopelekea watu wengi kukumbwa na baa la njaa duniani. Umefika wakati kwa Jumuiya ya Kimataifa kujifunga kibwebwe kukuza soko la uwekezaji utakaokuwa na mafao kwa jamii, ili kudhibiti uchumi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu.

Baba Mtakatifu anasema, tarehe 16 Juni, Kanisa linafanya kumbu kumbu ya Mashahidi Quirico na Julitta, Mtoto na Mama, ambao wakati wa madhulumu ya Dioklesiani, waliacha mali yao yote na kwenda kukabiliana na kifo, mwaliko wa kuchuchumilia mafao ya wengi, kwa kuonesha upendo na mshikamano kwa maskini na wanyonge ndani ya jamii







All the contents on this site are copyrighted ©.