2014-06-17 12:28:07

Mafisadi wanaangamiza maisha ya watu, njia pekee ni kutubu!


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, Jumanne, tarehe 17 Juni 2014 anasema: rushwa, ufisadi, mauaji na nyanyaso dhidi ya wanyonge kama ambavyo Mfalme Ahabu wa Israeli alivyomtenda Nabothi ni mambo yanayomkasirisha sana Mwenyezi Mungu na mwaliko kwa watu kama hawa ni kutubu dhambi zao ili kuonja tena huruma na upendo wa Mungu, vinginevyo hasira ya Mungu itawaka juu yao!

Mafisadi wa aina zote ni watu ambao wanawafanya watu wa Mungu kutenda dhambi na hivyo kumkasirisha Mwenyezi Mungu. Yesu katika mafundisho yake anaonya watu ambao wanakuwa ni kikwazo kwa Jamii, kuwa makini kwani wanaweza kuonja hasira ya Mungu kama inavyojionesha kwenye Liturujia ya Neno la Mungu kutoka katika Kitabu cha kwanza cha Wafalme, Sura ya 21:17 - 29.

Lakini pia Baba Mtakatifu anaonya kwamba, kama mtu hana uhakika kuhusu ufisadi na vitendo vya rushwa au mauaji yaliyofanywa na mtu ni vyema kukaa kimya kwani kumhukumu kwamba, ni fisadi ni sawa na kumwondosha machoni pa Mungu. Kwa wale wanaoiba, wanaoua na kuwanyanyasa maskini, watakiona cha mtema kumi mbele ya Mwenyezi Mungu.

Mfalme Ahabu aliposikia hasira ya Mungu imemwakia, alitubu na kujinyenyekesha mbele ya Mungu kwa kuomba msamaha wa dhambi zake. Hii ndiyo njia mafisadi ndani na nje ya Kanisa wanapaswa kuifuata, kama alivyofanya Zakayo Mtoza ushuru aliyekutana na Yesu akatubu na kuongoka, akarudisha mali aliyokuwa ameiba na hivyo kuanza maisha mapya.

Kwa mafisadi, wala rushwa na wauaji wasiotubu watakufa wakiwa wameelemewa na dhambi zao mioyoni mwao. Watu wana haki ya kulaani na kuwashutumu mafisadi, lakini pia wawe na ujasiri wa kuomba neema kutoka kwa Mungu ili nao wasitumbukie katika mtindo huo wa maisha, na hatimaye, wakakiona cha mtema kuni mbele ya Mwenyezi Mungu!







All the contents on this site are copyrighted ©.