2014-06-17 11:50:21

Kanisa halina budi kuwa huru ili kuonesha ujasiri!


Askofu mkuu Justin Welby wa Jimbo kuu la Cantebury ambaye pia ni kiongozi mkuu wa Jumuiya ya Kanisa Anglikani duniani wakati alipokuwa anazungumza na Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 16 Juni 2014 mjini Vatican amesema kwamba, Kanisa halina budi kuwa huru na kuonesha ujasiri wa kusimama kidete kulinda na kutetea amani, utu na heshima ya binadamu dhidi ya biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo; mambo ambayo yanaendelea kumdhalilisha binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Kuna maelfu ya watu wanaoendelea kutolea ushuhuda wa maisha yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, hali aliyojionea mwenyewe kwenye kumbu kumbu zinazohifadhiwa kwenye Kanisa kuu la Mtume Bartolomeo lililoko mjini Roma. Ushirikiano kati ya Kanisa Katoliki na Kanisa Anglikana unaweza kusaidia katika mchakato wa mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu na kwamba, hii ni neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya waja wake, kumbe wanapaswa kuitumia kikamilifu, ili kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu.

Askofu mkuu Justin Welby amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa ujasiri na ushuhuda aliouonesha hivi karibuni kwa kuwaalika Marais wa Palestina na Israeli kusali kwa pamoja ili kuombea amani na upatanisho huko Mashariki ya Kati. Umoja na ushirikiano miongoni mwa Makanisa inaweza kuwa ni changamoto katika kulinda, kutetea na kudumisha amani sehemu mbali mbali za dunia.

Askofu mkuu Welby amempongeza Baba Mtakatifu kwa misaada ya hali na mali anayoendelea kutoa kwa ajili ya maendeleo ya watu wa Amerika ya Kusini pamoja na mchakato wa majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Makanisa. Jambo la msingi ni kuangalia mambo yanayounganisha Makanisa haya mawili kuliko yale ambayo ni kikwazo na mwendelezo wa utengano.

Novemba mwaka 2014, Kanisa Katoliki litaadhimisha kumbu kumbu ya miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha Waraka kuhusu Majadiliano ya Kiekumene, Unitatis Redintegratio. Na mwaka 2016 itakuwa ni kumbu kumbu ya Miaka 50 tangu tangu Askofu mkuu Ramsey alipomtembelea Papa Paulo VI na kumzawadia pete yake ya kipapa.

Askofu mkuu Welby anasema, kuna ushirikiano mkubwa kati ya Kanisa Anglikani na Kanisa katoliki nchini Uingereza, kwani wamekuwa na fursa mbali mbali za kusali, kuamua na kutenda kwa kushirikiana na Kardinali Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza.







All the contents on this site are copyrighted ©.