2014-06-16 09:27:35

Mungu ni upendo, pendaneni ninyi kwa ninyi!


Sherehe za Fumbo la Utatu Mtakatifu ni mwaliko kwa waamini kutafakari na kumwabudu Mungu Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, wanaonesha maisha ya umoja na upendo mkamilifu, chanzo na kilele cha viumbe vyote. Kwa njia ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, waamini wanapata fursa ya kutambua muundo wa Kanisa ambalo waamini wanaalikwa kulipenda kama Yesu mwenyewe alivyowapenda upeo! Ni upendo unaonesha imani katika Fumbo la Utatu Mtakatifu.

Hii ni sehemu ya tafakari iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 15 Juni 2014 wakati wa Sherehe ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Anasema, upendo ni kielelezo makini cha Ukristo unaonesha urafiki wao na Yesu Kristo. Chuki, kinzani na uhasama ni mambo ambayo kimsingi yanapinga na Ukristo kwani Mungu ni upendo.

Waamini wote wanachangamotishwa na Mama Kanisa kutangaza na kushuhudia kwamba, Mungu ni upendo na anafanya hija na watu wake katika shida na mahangaiko yao; katika furaha na raha. Mwenyezi Mungu ameupenda hivi ulimwengu hata akatwaa mwili na kufanyika mwanadamu, ili aweze kuukomboa ulimwengu kwa njia ya Yesu Kristo. Huu ndio ule upendo unamwezesha Mwenyezi Mungu kusamehe na kwa njia ya Yesu Kristo, waamini wanaonja upendo wa Mungu.

Roho Mtakatifu ni zawadi ya Yesu Kristo Mfufuka, anayewakirimia waja wake maisha mapya na kuwawezesha kushiriki katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, katika upendo, umoja, huduma makini na kushirikishana. Mtu anayependa kwa sababu ya upendo wenyewe anaonesha ile taswira ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Hivi ndivyo ilivyo pia kwa familia na kwa parokia katika ujumla wake, kwani watu wanapopendana na kushirikishana mambo ya kiroho na kimwili, wanaonesha ile taswira ya Fumbo la Utatu Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anasema, huu ni upendo usiokuwa na mipaka, upendo unaoheshimu uhuru wa wengine na kwamba, kila Jumapili, waamini wanaadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu, kielelezo cha moto wa upendo, hapa linaishi Fumbo la Utatu Mtakatifu. Hii ndio maana Kanisa linaadhimisha Siku kuu ya Ekaristi Takatifu mara baada ya kuadhimisha Fumbo la Utatu Mtakatifu.

Alhamisi, ijayo, tarehe 19 Juni 2014 Baba Mtakatifu Francisko anasema anatarajia kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na baadaye kufanya maandamano ya Ekaristi Takatifu kutoka kwenye Kanisa kuu la Yohane wa Laterano hadi kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu lililoko mjini Roma. Anawaalika waamini na mahujaji kushiriki kwa wingi katika tukio hili la imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.