Kumhudumia maskini ni kugusa Madonda Matakatifu ya Yesu!
Professa Andrea Riccardi mwanzilishi wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye makao yake
makuu mjini Roma wakati akitoa hotuba ya makaribisho kwa Baba Mtakatifu Francisko
alipotembelea Jumuiya hiyo, Jumapili tarehe 15 Juni 2014 anasema, ni ndoto ya Jumuiya
yake kuwa ni Kanisa kwa ajili ya wote, lakini zaidi kwa kutoa kipaumbele kwa maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Wanataka kuchangia katika mchakato
wa mabadiliko duniani kwa kusikiliza kwa makini Neno la Mungu, kwa kutoa kipaumbele
cha kwanza kwa Yesu na binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Wanataka kudumisha
misingi ya haki, amani na upatanisho, muujiza ambao unawezekana kwa njia ya imani,
sala na majadiliano ya kweli. Kwa hakika anasema Professa Riccardi inapendeza kuwa
Mkristo.
Baba Mtakatifu akiwa kwenye Kanisa la Bikira Maria wa Trastevere mjini
Roma alipata nafasi ya kusikiliza shuhuda zilizotolewa na watu wanane wanaowakilisha
makundi ya wale wanaohudumiwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yaani: Wazee, wakimbizi,
maskini, walemavu na watu wasiokuwa na fursa ya ajira.
Askofu mkuu Jean Kawak
wa Kanisa la Kiorthodox, Jimbo kuu la Damasko anasema kuna viongozi mbali mbali wa
kidini wametekwa nyara nchini Syria na wanaendelea kuteseka na kwamba, Kanisa linasubiri
kwa imani na matumaini siku ambayo wataachiliwa huru. Wananchi wa Syria wanateseka
kutokana na baa la njaa, magonjwa, ukosefu wa fursa za ajira na umaskini. Takwimu
zinaonesha kwamba, zaidi ya watu 160, 000 wamefariki dunia katika vita inayoendelea
nchini Syria. Pamoja na changamoto zote hizi watu bado wana imani na matumaini ya
Syria bora zaidi.
Bibi Irma Lombardi, mwenye umri wa miaka 90 amemshukuru Baba
Mtakatifu Francisko kwa kuonesha upendo pamoja na kuwajali wazee kinyume kabisa cha
utamaduni unaoendelea kujengeka kwa sasa wa kutowathamini wala kuwajali wazee. Jumuiya
ya Mtakatifu Egidio kwa muda wa miaka 20 imemsaidia kuonja upendo na ukarimu wa Familia
ya Mungu na kwamba, kuwa mzee si dhambi bali ni sehemu ya mchakato wa maisha. Kanisa
lijenge utamaduni wa kuwasaidia na kuwahudumia wazee hasa katika maisha yao ya kiroho.
Kuwasaidia maskini ni kugusa Madonda Matakatifu ya Yesu.
Vijana wanasema wao
wanapenda kushiriki katika Jumuiya ya Mtakatifu Egidio ili kudumisha misingi ya haki
na amani, kwa kuwasaidia na kuwahudumia wazee na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa
Jamii, ili kutambua na kuthamini utu wao kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano
wa Mungu. Kwa kusaidiana kuwawawezesha watu kupata chemchemi ya maisha.
Baadhi
ya watu wasiokuwa na fursa za ajira wanasema, wana familia na watoto, wanakosa furaha
ya kweli kwa vile hawana ajira na fedha za kuweza kuhudumia familia zao. Athari za
myumbo wa uchumi kimataifa zimepelekea watu wengi kukosa ajira kiasi kwamba, utu wao
umewekwa rehani.
Baadhi ya watu katika ushuhuda wao wanasema, maisha yao yamebadilika
kwa haraka baada ya kuwapoteza wazazi, wenzi na wapendwa wao. Lakini kwa njia ya marafiki
wema na watakatifu wameweza kuwasaidia kuonje furaha na matumaini tena katika maisha,
kiasi kwamba, hata wao wanapenda kuwahudumia wengine kama alama ya shukrani. Hakuna
furaha kubwa kama kujenga urafiki na Yesu, kwa kusikiliza Neno pamoja na kushiriki
Sakramenti za Kanisa. Leo hii wanayo furaha ya kuwatangazia wengine Injili ya Furaha
kwa njia ya ushuhuda wa huduma!
Baadhi ya watu wanaohudumiwa na Jumuiya ya
Mtakatifu Egidio mjini Roma wanasema, kutokana vita, dhuluma na kinzani za kijamii
wamelazimika kuzikimbia nchi zao na sasa wanaishi katika mazihngira hatarishi, lakini
wameona mwanga wa amani na utulivu kutoka katika Jumuiya ya Mtakatifu Egidio. Kuna
haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutafuta na hatimaye kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo
la Zingari wanaolazimika kuishi mafichoni na hivyo kuendelea kunyanyasika na kwamba,
hata wao wanawajibika kuwa wajenzi wa haki na amani katika Jamii inayowapatia hifadhi.
Baadhi
ya wakimbizi wanasema, wamelazimika kuzikimbia nchi zao kutokana na vita na dhuluma
za kikabila, ambazo zinawafanya wakati mwingine kuamua kuchukua maamuzi magumu katika
maisha. Safari ya kutafuta maisha bora ughaibuni ina gharama na magumu yake; ina hatari
na hasara zake; daima kifo kiko mkononi! Ameshuhudia baadhi ya rafiki zake wakifa
maji bila msaada wowote ule. Ni safari ya hatari, chini ya uvungu wa gari kwa muda
wa masaa 35! Baadhi ya vijana wanashindwa kuvumilia na hivyo wanajikuta wakianguka
barabarani na kugongwa na magari! Hata wakimbizi na wahamiaji wanatamani kuona amani
na utulivu vikitawala nchini mwao!
Imehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.