Syria inahitaji misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa!
Viongozi wa wanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni hivi karibuni walifanya mkutano
chini ya uongozi wa Patriaki Karekin wa Pili, Kiongozi mkuu wa Waamini Wakatoliki
wa Armenia, ili kuangalia kwa pamoja changamoto za kiimani zinazoendelea kujitokeza
nchini Syria kwa wakati huu.
Kwa pamoja wanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni
wameomba kuondolewa kwa vikwazo vya kugharimia huduma za kibinadamu zinazotolewa na
Mashirika ya Misaada Kimataifa; kusitisha biashara haramu ya silaha inayoendelea kusababisha
maafa makubwa kwa watu na mali zao pamoja na kuondoa majeshi ya kukodiwa kutoka nje
ya Syria yanayoendesha vita nchini humo!
Baraza la Makanisa Ulimwenguni linaendelea
kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kusaidia mchakato wa upatikanaji wa amani na utulivu
nchini Syria baada ya mazungumzo ya awamu ya kwanza na ile ya pili mjini Geneva kushindwa
kuzaa matunda yaliyokuwa yanakusudiwa. Wakimbizi na wahamiaji kutoka Syria wanaoishi
katika nchi jirani wapatiwe misaada ya kibinadamu. Ni wajibu wa viongozi na wadau
mbali mbali wa Syria kuanza kujitika katika upatanisho wa kitaifa kwa kujenga na kuimarisha
misingi ya haki na amani.
Baraza la Makanisa Ulimwenguni limewataka wale waliowateka
nyara Maaskofu kutoka Aleppo kuwaachilia maramoja pasi na masharti ili waweze kuungana
na ndugu zao katika kutoa huduma za kichungaji.