2014-06-14 11:30:27

Mkutano wa kimataifa dhidi ya Boko Haram!


Jumuiya ya Kimataifa imeamua kuwavalia njuga wanajeshi wa Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram kinachoendelea kusababisha maafa makubwa kwa wananchi wasiokuwa na hatia ndani na nje ya Nigeria. Mawaziri wa mambo ya Nchi za Nje kutoka Uingereza, Benin, Cameroon, Ciad, Niger, Umoja wa Ulaya, Canada na Marekani, Ijumaa tarehe 13 Juni 2014 wamekutana na kujadili tatizo hili na changamoto zake katika kulinda na kudumisha amani na usalama nchini Nigeria na katika nchi jirani ambao pia wanatishiwa na mashambulizi ya kigaidi kutoka kwa Kikundi cha Boko Haram.

Mawaziri hawa walikuwa wanashiriki katika mkutano wa kimataifa uliokuwa unatafuta mbinu za kupambana na hatimaye kusitisha kabisa nyanyaso za kijinsia katika maeneo ambamo vita inaendelea kurindima. Jumuiya ya Kimataifa inaendelea kuonesha mshikamano wa hali na mali katika harakati za kutaka kuokoa maisha ya wasichana waliotekwa nyara na Boko Haram, Kaskazini mwa Nigeria.

Uingereza itaongeza msaada wake wa kijeshi na huduma katika sekta ya elimu nchini Nigeria, ili amani na utulivu viweze kurejea tena!







All the contents on this site are copyrighted ©.