2014-06-14 10:18:53

Gawio la Tanzania kutoka TIPER kuelekezwa katika sekta ya elimu, afya na maji


Serikali ya Tanzania imepokea shilingi bilioni moja kutoka TIPER ikiwa ni gawio ambalo kampuni hiyo imekuwa ikilipa kwa Wanahisa wake kila mwaka. Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Dkt. Servarcius Likwelile alipokuwa akipokea gawio hilo katika hafla iliyofanyika Ijumaa tarehe 13 Juni 2014 mjini Dodoma.


Dkt. Likwelile alisema kuwa gawio hilo litaelekezwa kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha 2013/2014 unaomalizika kwa kuangalia maeneo ambayo yanawagusa wananchi ikiwemo sekta ya elimu, afya na maji. Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Daniel Belair alisema kuwa si mara ya kwanza kwa kampuni yake kutoa gawio kama hilo kwa Serikali ambapo mwaka jana muda kama huu kampuni ilitoa kiasi kama hicho kama gawio.


Mkurugenzi huyo alisema kuwa kampuni yake imeendelea kufanya vizuri katika kukuza maisha ya kijamii na kiuchumi ambapo kwa sasa inafanyakazi kwa saa 24 na siku saba za wiki. Kwa kuzingatia utendaji huo, kampuni ya TIPER imekuwa kichocheo kukuu cha kuzalisha ajira nchini ambapo hadi sasa asilimia 99 ya wafanyakazi wake ni nguvu kazi ya Watanzania.


Naye Mwenyekiti Mtendaji wa Bodi ya Wakurugenzi ya TIPER Prof. Abdulkarim Mruma alisema kuwa imekuwa ni muhimu kwa kampuni yao kuwa na akiba ya kutosha ya mafuta kwa nchi na kuleta mafanikio makubwa ya upatikanaji wa mafuta nchini. Aidha, TIPER Prof. Mruma alisema kuwa kwa sasa kampuni yao imejikita katika kuleta mafuta yaliyosafishwa nchini ili kupunguza gharama zisizokuwa za lazima.


“Kwa sasa tunaleta mafuta yaliyosafishwa badala ya mafuta ghafi ambayo yanazalisha tope jingi ambalo limekuwa ni hatari katika kutunza mazingira yetu” alisema Prof. Mruma. Pamoja na ufanisi huo, kumekuwepo na changamoto za kuboresha mkataba wa utendaji na usimamizi wa hesabu masuala ambayo wanahisa wote wawili wanaendelea kuyafanyia kazi kwa madhumuni ya kuwa na matokeo mazuri zaidi kwa pande zote.


Kiutendaji kampuni ya TIPER inaendeshwa kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania ambayo ina hisa zenye asilimia 50 na Kampuni ya Oryx Energies SA asilimia 50. Pamoja na Tanzania Kampuni ya Oryx Energies SA inafanyakazi katika nchi mbalimbali duniani ambazo ni Benin, Burkina Faso, Côte d'Ivoire, Guinea Conakry, Kenya, Mali, Niger, Nigeria, Senegal, Sierra Leone, Afrika Kusini, Hispania (Visiwa vya Canary), Togo, Uganda na Zambia.








All the contents on this site are copyrighted ©.