Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria katika ujumbe wake uliotolewa kwa vyombo vya habari
hivi karibuni linasema kwamba, dini ni sawa na upanga wenye makali kuwili, inaweza
kutumika kwa ajili ya kuwajenga na kuwaimarisha watu katika umoja na mshikamano wa
kitaifa kwa kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi. Dini pia inaweza kutumiwa
vibaya kuwagawa, kuwanyanyasa na kuwadhulumu watu na matokeo yake ni machafuko ya
kidini na maafa kwa watu wasiokuwa na hatia!
Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria
linasema kwamba, changamoto kubwa iliyoko mbele ya wananchi wa Nigeria ni kuweza kuweka
uwiano mzuri katika masuala ya kidini, ustawi na maendeleo ya watu. Jambo hili linawezekana
ikiwa kama Katiba ya nchi ambayo ni sheria mama itatekelezwa kikamilifu. Katiba inatambua
kwamba, Nigeria ni nchi ambayo ina amini katika uwepo wa Mungu mmoja na kwamba Serikali
kuu au Serikali za Kijimbo hazitaruhusiwa kuwa na dini kama dini ya Jimbo au Nchi
ya Nigeria.
Kumbe, baadhi ya wanasiasa kuchukulia kwamba, Uislam ndiyo dini
rasmi ya Majimbo yaliyoko Kaskazini mwa Nigeria ni kwenda kinyume cha Katiba ya nchi
na matokeo yake ni kuendelea kushuhudia maafa ya watu wasiokuwa na hatia wanaoendelea
kupoteza maisha yao kutokana na misimamo mikali ya kidini. Hali hii imepelekea hata
kuwepo kwa sheria na sera za kibaguzi zinazotekelezwa na Serikali za Majimbo kiasi
kwamba, Wakristo hawana haki ya kununua ardhi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za ibada
na kwamba, wanatengwa hata katika ufadhili wa masuala ya hija za maisha ya kiroho!