2014-06-12 07:59:19

Mada zitakazojadiliwa kwenye Mkutano mkuu wa AMECEA


Kamati tendaji ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA chini ya Katibu mkuu wa AMECEA, Padre Ferdinand Lugonzo imetoa mada zitakazojadiliwa wakati wa maadhimisho ya Mkutano mkuu wa 18 wa AMECEA utakaofanyika nchini Malawi kuanzia tarehe 16 hadi tarehe 26 Julai 2014 kwa kuongozwa na kauli mbiu “Uinjilishaji kwa njia ya wongofu na ushuhuda wa Imani ya Kikristo”. RealAudioMP3

Wajumbe watashirikishwa mada inayojadili “Kazi za awali za kimissionari na hali halisi katika Ukanda wa AMECEA. Ni mada itakayowasilishwa na wajumbe kutoka Uganda. Wajumbe kutoka Sudan katika ujumla wao, watajadili kuhusu mazingira ya kitamaduni, kisiasa, kijamii ambamo Kanisa linaendelea kutekeleza utume wake.

Wajumbe kutoka Tanzania wamepewa mada mbili za kujadili: mosi ni kuhusu Uinjilishaji kama fursa inayowawezesha waamini kujikita katika wongofu na ushuhuda wa imani ya Kikristo kwa kuweka mkazo katika maisha ya familia na jumuiya ndogo ndogo za Kikristo. Mada ya pili itaangalia kwa namna ya pekee kabisa athari za teknolojia ya digitali na njia za mawasiliano katika utume wa Uinjilishaji unaofanywa na Kanisa.

Wajumbe kutoka Zambia wamepangiwa kushirikisha umuhimu wa Seminari na nyumba za malezi katika kukuza Uinjilishaji Mpya na Malawi ambayo ni mwenyeji wa maadhimisho ya Mkutano mkuu wa 18 wa AMECEA kwa Mwaka 2014 watashirikisha kuhusu umuhimu wa huduma za kiroho na taasisi za elimu ya juu katika kuendeleza Uinjilishaji Mpya.

Wajumbe wa AMECEA kutoka Kenya watapembua kwa kina na mapana kuhusu Liturujia na Utamadunisho kama njia za Uinjilishaji. Kimsingi mada saba ndizo zitakazofanyiwa kazi na wajumbe wapatao 300 kutoka ndani na nje ya Nchi za AMECEA. Wajumbe watapata fursa pia ya kuchangia katika majadiliano, ili kupata uelewa mkubwa zaidi.

Maaskofu wataweza kuibua mikakati ambayo wataifanyia kazi katika mchakato wa kuimarisha shughuli za kichungaji zinazotekelezwa na Kanisa katika nchi za AMECEA.








All the contents on this site are copyrighted ©.