Taarifa za kidemografia, kijamii na kiuchumi Tanzania
Ifuatayo ni hotuba iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania tarehe 10 Juni 2014
wakati wa uzinduzi wa chapisho la tatu la taarifa za msingi za kidemografia, kijami
na kiuchumi linalotokana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.
Shukrani
na Pongezi
Ndugu Wananchi; Awali ya yote, naomba tuanze kwa kumshukuru
Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima na kutuwezesha kukutana hapa siku
ya leo. Napenda pia kuwashukuru waandaaji wa hafla hii kwa kunipa heshima kubwa ya
kuzindua Chapisho la Tatu la Taarifa za Msingi za Kidemografia, Kijamii na Kiuchumi
Linalotokana na Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012.
Nakushukuru sana Mheshimiwa
Waziri Mkuu kwa maelezo yako mazuri ya awali kuhusu Chapisho hili. Nakupongeza wewe,
pamoja na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa uongozi wenu mzuri wa zoezi la Sensa.
Chapisho tunalozindua leo ni matunda ya kazi nzuri mliyoifanya ya kuziongoza Idara
za Takwimu za Serikali zetu mbili ambazo ndizo zilizosimamia na kuendesha zoezi lenyewe
la sense ya watu na makazi.
Sensa inaendeshwa kwa mujibu wa kifungu cha 14
cha Sheria ya Takwimu (the Statistic Act) sura ya 351. Katika kipindi chote cha miaka
50 ya Muungano wetu tumefanya Sensa mara tano, mwaka 1967, 1978, 1988, 2002 na 2012.
Umuhimu wa Chapisho la Tatu
Ndugu Wananchi;
Sensa ni
zoezi pana sana. Sensa ni zaidi ya kuhesabu watu. Sensa hujumuisha pia kukusanya na
kufanya uchambuzi wa taarifa kuhusu masuala mbalimbali ya kiuchumi na kijamii. Taarifa
hizo husaidia Serikali katika utungaji wa sera na kutengeneza mipango na mikakati
ya maendeleo nchini. Tangu kufanyika kwa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012, Idara
Kuu ya Takwimu ya Taifa na Idara ya Takwimu Zanzibar ambazo ndizo zilizohusika na
zoezi hili zimeendelea kutoa matokeo kulingana na kalenda ya utoaji wa matokeo ya
Sensa. Matokeo ya mwanzo nilitolewa tarehe 31 Desemba, mwaka 2012 kwenye viwanja vya
Mnazi Mmoja. Siku ile nilitangaza jumla ya idadi ya watu nchini Tanzania. Chapisho
la pili lilihusu mgawanyo wa watu kwa umri na jinsi ambalo lilitolewa tarehe 25 Septemba,
2013.
Chapisho la Tatu ninalolizindua leo linatoa taarifa za msingi za kidemografia
(mnyumbuliko wa idadi ya watu), kijamii na kiuchumi zinazotokana na Sensa ya Watu
na Makazi ya mwaka 2012. Taarifa za Chapisho la Tatu zina umuhimu wa aina yake. Zinaonesha
Tanzania imepiga hatua kiasi gani katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Aidha,
upatikanaji wa taarifa katika kipindi hiki utaviwezesha vizazi vijavyo kuifahamu Tanzania
ilivyokuwa mwaka 2012.
Muhtasari wa Matokeo ya Chapisho la Tatu
Ndugu
Wananchi;
Sensa ya Mwaka 2012 imefanyika katikati ya utekelezaji wa Mpango
wa Taifa wa Miaka 5 (2011-2016). Mpango huu tunaoendelea kuutekeleza una lengo la
kutufikisha kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025 na ile ya Zanzibar ya
mwaka 2020 ambapo tunatarajia kuwa nchi yetu itakuwa imefikia uchumi wa kati. Kwa
utaratibu huu wa kufanya Sensa kila baada ya miaka 10, ina maana kuwa Sensa inayofuata
itafanyika mwaka 2022 ikiwa ni miaka michache kabla ya kufikia Dira ya Taifa. Hivyo,
matokeo haya ni msingi wa kupima mwelekeo wetu kiuchumi na kijamii kufikia lengo letu
la kuwa uchumi wa kati ifikapo 2020 kwa upande wa Zanzibar na 2025 nchi nzima.
Chapisho
hili lina takwimu nyingi sana kuhusu nyanja mbalimbali za maisha ya Watanzania. Takwimu
hizi zinatupa fursa ya kujua maeneo tunayofanya vizuri na yale tunayohitajika kuyaimarisha.
Vilevile, zinatuonyesha yale maeneo ambayo tulidhani tunafanya vizuri lakini kumbe
siyo, hivyo basi tunatakiwa kuyawekea mkakati maalum. Hali kadhalika, taarifa zinatuamsha
kuona yale maeneo mapya ambayo hatukuwahi kuyafikiria lakini sasa tunapaswa kuyaangalia
kwa karibu.
Kwa ujumla, kulingana na takwimu za Sensa ya 2012, idadi ya watu
Tanzania iliongezeka kutoka watu milioni 34.4 mwaka 2002 hadi watu milioni 44.9 mwaka
2012. Hii ni sawa na kasi ya ongezeko la asilimia 2.7 kwa mwaka. Kwa kasi hii ya ongezeko
la watu, Tanzania Bara inatarajiwa kuwa na watu milioni 63.3 mwaka 2025 ambao ndiyo
mwaka wa mwisho wa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo 2025 kwa Tanzania Bara. Aidha,
Zanzibar inatarajiwa kuwa na watu milioni 1.8 ifikapo mwaka 2020 ambao ndiyo mwaka
wa mwisho wa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Zanzibar. Kwa kasi hii ya ongezeko
la idadi ya watu Tanzania inatarajiwa kuwa na watu milioni 125 mwaka 2050.
Ndugu
Wananchi;
Ili kufikia dira zetu za maendeleo, yaani ya mwaka 2020 kwa Zanzibar
na ya mwaka 2025 kwa nchi nzima ambapo tutakuwa na idadi ya watu takribanimilioni
65.1, inatupasa kujitazama tulipotoka na tulipo leo. Kwa mujibu wa Chapisho hili la
Tatu, tumepiga hatua kubwa na nzuri katika maeneo mengi, na hivyo kuashiria kuwa tuko
katika mstari sahihi kuelekea Tanzania tunayoitamani. Baadhi ya takwimu hizi kwa ufupi
ni zifuatazo:
Zaidi ya asilimia 90 ya watu wote Tanzania walizaliwa
baada ya Muungano wa mwaka 1964. Tafsiri yake ni kwamba idadi kubwa ya Watanzania
ni vijana ambao wamezaliwa, kukua na kufaidika na matunda ya Muungano. Hiki ni kiashiria
kikubwa kuwa tumeweza kujenga utaifa mpya, yaani utanzania katika miaka 50 ya Muungano
wetu.
Hii ni Sensa ya tano tangu Muungano wetu
mwaka 1964. Sensa ya kwanza ilikuwa mwaka 1967, ya pili mwaka 1978, ya tatu mwaka
1988, ya nne mwaka 2002 na ya tano 2012. Takwimu za Sensa za kati ya mwaka 1967 na
mwaka 2012 zinaonesha kuwa idadi ya watu waTanzania ambao wanaishi mijini imeongezeka
kutoka asilimia6 mwaka 1967 hadi asilimia 30 mwaka 2012. Ukuaji huu wa miji ni kiashiria
muhimu kuwa safari yetu ya kuelekea uchumi wa katini ya uhakika. Hatuna budi sasa,
sera na mikakati yetu kuielekeza katika kuhakikisha miji yetu inao uwezo wa kuhimili
ongezeko hili la watu kwa maana ya utoaji wa huduma za kijamii na ajira.
Katika kipindi cha miaka 50 wastani wa umri wa kuishi kwa
mtoto wa Kitanzania anayezaliwa umeongezeka kutoka miaka 41 mwaka 1967 hadi kufikia
miaka 61 mwaka 2012. Maana yake ni kuwa, huduma za afya zimeimarika, watu sasa wanaishi
kwa muda mrefu zaidi kuliko ilivyokuwa awali. Hata hivyo, bado hatujafikia viwango
vya wenzetu wa Asia na Ulaya ambao wastani wao ni miaka 70 na kuendelea.
Vifo vya watoto wachanga vimepungua kutoka vifo 115 kati ya kila
watoto 1,000 wanaozaliwa hai mwaka 1988 hadi kufikia vifo 45 mwaka 2012. Na, mwaka
2013 tumefikia 21. Vifo vya watoto chini ya miaka 5 vimepungua kutoka 231 mwaka 1988
hadi 68 mwaka 2012 na 2013 tumefikia vifo 54 kwa 1,000. Pia, idadi ya vifo vitokanavyo
na uzazi imepungua kutoka vifo 578kwa kila akina mama 100,000 wanaojifungua mwaka
2004/2005 hadi 454 mwaka 2010 na kwa mujibu wa takwimu za Sensa, vifo hivi vimeendelea
kupungua hadi 432 mwaka 2012. Hii ni hatua kubwa kuelekea lengo la Milenia ya Mwaka
2015 ya vifo 193.
Asilimia ya kaya zinazopata
maji safi ya kunywa imefikia asilimia 57 mwaka 2012. Vile vile, kaya zinazotumia umeme
kama nishati ya kuangazia zimeongezeka kutoka asilimia 10 mwaka 2002 hadi asilimia
21 mwaka 2012.
Kwa upande wa sekta ya elimu,
asilimia ya watu wenye umri wa miaka 10 na zaidi wanaojua kusoma na kuandika kwa Tanzania
Bara imeongezeka kutoka asilimia 31 mwaka 1967 hadi kufikia asilimia 78 mwaka 2012.
Kwa Zanzibar kiwango hiki kimeongezeka kutoka asilimia 39 mwaka 1967 hadi asilimia
86mwaka 2012.
Takwimu zinazoonesha kwamba
umaskini wa kipato umepungua kutoka asilimia 33.6 mwaka 2007 hadi asilimia 28.2 mwaka
2012.
Takwimu zinaonesha kwamba makazi ya wananchi
wote wa Tanzania yaliyojengwa kwa vifaa vya kisasa (zege, mawe, saruji na vyuma) yameongezeka.
Familia zinazoishi kwenye nyumba za bati zimeongezeka kutoka asilimia 46mwaka 2002
hadi asilimia 65 mwaka 2012.
Vilevile, umiliki
wa simu za kiganjani umeongezeka sana. Mwaka 2012 wastani ulikuwa ni asilimia 64ikilinganishwa
na asilimia 10 mwaka 2005. Kuongezeka kwa simu ni kiashiria cha kuongezeka kwa biashara,
idadi ya watu wanaotumia huduma za kifedha kwa njia ya simu na urahisi wa mawasiliano
ambao unawezesha usambazaji wa taarifa za kijamii na kibiashara katika maeneo mengi
hivi sasa.
Mazingatio Yatokanayo na Chapisho la Tatu la Sensa
Ndugu
Wananchi;
Ufupi au urefu wa safari unaweza kuujua tu iwapo unafahamu unapotoka,
ulipo na unapokwenda. Taarifa ambazo zimewasilishwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu zinaonesha
kuwa tumepata mafanikio ya kuridhisha katika maeneo mengi, na kuwa tumekuwa tunasonga
mbele mwaka hadi mwaka na siyo kurudi nyuma. Kwa hiyo matokeo haya yanapaswa kuwaongoza
Viongozi na Watendaji wa ngazi zote katika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa kujua
maeneo ambayo kasi ya utekelezaji wa programu za maendeleo kwa wananchi ilikuwa ndogo,
na hivyo kustahili kupewa msukumo mpya katika utekelezaji wake.
Ndugu Wananchi;
Nimefarijika
kusikia kuwa taarifa za Sensa zinaonesha hatua kubwa tuliyopiga katika kuleta usawa
wa kijinsia kati ya wanaume na wanawake. Ingawa viashiria vingi bado vinaonekana bora
zaidi kwa wanaume kuliko wanawake, lakini pengo kati yao limepungua ukilinganisha
na miaka ya nyuma. Kwa mfano, asilimia ya wanaume wenye umri wa miaka 10 na zaidi
wanaojua kusoma na kuandika ilikuwa asilimia 45 kwa Tanzania Bara na asilimia 55 kwa
Zanzibar mwaka 1967. Kwa upande wa wanawake ilikuwa asilimia 19 na asilimia 23 kwa
Tanzania Bara na Zanzibar mwaka 1967. Taarifa za Sensa ya Mwaka 2012 zinaonesha kuwa
pengo hili limepungua sana. Wanaume wenye umri wa miaka 10 na zaidi wanaojua kusoma
na kuandika kwa mwaka 2012 ni asilimia 82 ya wanaume wote kwa Bara ukilinganisha na
asilimia 75 kwa wanawake. Kwa upande wa Zanzibar, idadi ya wanaume wanaojua kusoma
na kuandika ni asilimia 89 ya wanaume wote kulinganisha na asilimia 83 ya wanawake.
Hatuwezi kupata maendeleo makubwa na endelevu bila kuhakikisha usawa wa kijinsia.
Wanawake ni asilimia 51 ya Watanzania wote, hivyo, hatuna namna yoyote tunayoweza
kulipuuza kundi hili kubwa, ambalo ni zaidi ya nusu ya idadi ya watu wote katika shughuli
za maendeleo. Ndiyo maana, tumeelekeza juhudi kubwa kurekebisha kasoro hii ya kihistoria
na kimfumo kwa kuwapa wanawake fursa ili nao washiriki sawia katika shughuli za maendeleo
katika ngazi ya familia, jamii na hata taifa. Ni vyema ikaeleweka kuwa hatuwapendelei
wanawake bali tunawapatia kile wanachostahili kupata kama raia na kama wanadamu. Stahili
ambazo wamekuwa wakizikosa kwa miaka mingi.
Serikali itaendelea kuimarisha
juhudi za utekelezaji wa Sera ambazo zinalenga kuhakikisha kuwa pengo hili linazibika
ili Watanzania wote wafaidike na rasilimali za Taifa bila ya kujali jinsia zao.
Maelekezo
kwa Tume ya Taifa ya Takwimu Ndugu Wananchi;
Nimesema hapo awali kuwa
lengo kubwa la kufanya Sensa ni kutoa takwimu ambazo zitachangia katika jitihada za
kuboresha maisha ya Watanzania. Taarifa za sensa ambazo zitasaidia kuboresha sera
za nchi kwa mambo mbalimbali, kupanga na kutathmini programu za maendeleo na uimarishaji
wa utoaji wa huduma za jamii. Lengo hili haliwezi kufikiwa ikiwa taarifa za sensa
na nyinginezo kwa ujumla wake hazitawafikia watumiaji wote wanaozihitaji. Ofisi za
Takwimu zina jukumu la kutoa takwimu katika mfumo mzuri na lugha rahisi na kuzisambaza
na kuhamasisha matumizi yake.
Pamoja na usambazaji wa taarifa za sensa kwa
vitabu na machapisho, tumieni tovuti na njia nyingine za kisasa kusambaza taarifa
zenu. Ninafarijika kusikia kwamba tayari mmeanza juhudi hizi, kwani uzinduzi wa Chapisho
hili la tatu utaenda sambamba na uzinduzi wa usambazaji wa taarifa kwa njia ya mtandao.
Ofisi za Takwimu zimetimiza wajibu wake wa kutoa takwimu na sasa ni jukumu
la Wizara, Idara,Taasisi za Serikali na watumiaji wengine wote kuzifanyia kazi. Natoa
agizo kwa viongozi ngazi zote za utawala kutafsiri matokeo haya kwa kuoanisha na utekelezaji
wa sera na programu za maendeleo ya kisekta katika maeneo yao. Matokeo haya ya Sensa
sasa ndiyo rejea yetu ya takwimu katika mipango yetu ya utekelezaji.
Kile
kisingizio cha kukosekana kwa takwimu mpya sasa kimefikia ukomo. Takwimu ni kitendea
kazi, sasa mnazo na mkazifanyie kazi, siyo kuendeleza semina za kujadili matatizo
na mapungufu. Takwimu zimetuonyesha mafanikio tuliyoyapata na mapungufu yaliyopo ambayo
mkayatatue na siyo kuyajadili.
Wito kwa Wananchi na Wadau Ndugu Wananchi;
Napenda
pia kutoa wito kwa wananchi na wadau wa maendeleo hasa asasi za kiraia kusoma taarifa
hizi na kuzitumia vizuri. Kumekuwepo na upotoshaji mkubwa sana wenye kubeza mafanikio
yaliyopatikana nchini kutokana na jitihada za Serikali na wananchi kwenye kuleta maendeleo.
Taarifa hii inaweka wazi ukweli ulivyo. Zitumieni. Kama upotoshaji ulikuwa ni kwa
sababu ya kukosekana kwa rejea ya takwimu sahihi, takwimu ndizo hizo kwa kila mmoja
wetu kuziona na kuzitumia. Asiyefanya hivyo ana lake jambo.
Hitimisho
Ndugu
Viongozi Wenzangu; Ndugu Wananchi;
Niruhusuni nirudie tena kuwashukuru washirika
wetu wa maendeleo waliotusaidia kufanikisha zoezi la Sensa ya watu na makazi. Kwa
namna ya pekee nawashukuru Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), Shirika la Maendeleo
la Uingereza (DFID), Taasisi za Umoja wa Mataifa ikiwemo UNFPA, UNDP na UNICEF. Nawashukuru
tena Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Pinda na Makamu wa Rais wa Zanzibar,
Balozi Ali Seif Idd kwa uongozi wenu mzuri uliowezesha zoezi zima la sensa kufanikiwa.
Pia, nawapongeza viongozi na watendaji wa Idara zetu mbili za Takwimu kwa kazi kubwa
na nzuri waliyofanya. Umakini na umahiri wao ndiyo uliotufikisha hapa.
Nawashukuru
na kuwapongeza viongozi wote wa Serikali wa ngazi zote za utawala ambao walishiriki
kwa ukamilifu katika maandalizi na hatimaye utekelezaji wa Sensa ya Mwaka 2012. Nitoe
pia shukrani kwa viongozi wa vyama vya siasa, madhehebu ya dini na mashirika yasiyo
ya Kiserikali kwa ushiriki wenu hasa kwenye hatua ya uhamasishaji wa ushiriki wa umma.
Nawashukuru wadau wetu wa maendeleo kwa michango yao muhimu ambayo imesaidia kufanikisha
sensa hii.
Shukrani za kipekee ziwaendee Wananchi wote ambao walijitokeza
kuhesabiwa na kujibu maswali ya sensa kwa ufahamu mkubwa. Kukubali kwao kushiriki
ndiko chanzo kilichowezesha kupatikana taarifa tunazozindua leo na nyingine zitakazofuata.
Ni dhahiri kuwa Serikali yetu imetimiza kwa ufanisi jukumu la kufanya Sensa ya Watu
na Makazi nchini. Lengo limetimia la kujua hali halisi ya rasilimali watu iliyopo
Nchini kama zilivyofanya Awamu zote zilizotangulia. Ndugu Wananchi;
Baada
ya kusema maneno haya ya utangulizi, sasa, kwa heshima na taadhima kubwa, napenda
kutamka kwamba Chapisho la Taarifa za Msingi za Kidemografia, Kijamii na Kiuchumi
linalotokana na Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012 Pamoja na Matumizi ya Tovuti
katika kupata taarifa mbalimbali za Sensa ya Watu na Makazi limezinduliwa rasmi.
Mungu
Ibariki Afrika! Mungu Ibariki Tanzania! Asanteni kwa kunisikiliza!