Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anawaalika
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuungana pamoja naye ili kuwaombea waathirika
wa nyanyaso za kijinsia na wale wanaotafuta njia muafaka ya kukomesha ukatili huu
sehemu mbali mbali za dunia. Huu ni muda wa kutenda!
Itakumbukwa kwamba, tarehe
10 hadi tarehe 13 Juni 2014 mjini London Serikali ya Uingereza imeitisha mkutano wa
kimataifa unaopania kutafuta mbinu za ukomeshaji wa nyanyaso za kijinsia katika maeneo
ambamo kuna vita na migogoro ya kijamii.
Mkutano huu unawashirikisha mawaziri
wa mambo ya nchi za nje, wanaharakati, vyama vya kiraia pamoja na viongozi wa kidini,
ili wote kwa pamoja waweze kujifunga kibwebwe kupambana na nyanyaso na ukatili wa
kijinsia unaodhalilisha utu na heshima ya binadamu!