2014-06-11 06:42:49

Eritrea kunawaka moto!


Ndugu yako uko wapi? Ndiyo kauli mbiu inayoongoza barua ya kichungaji ya Baraza la Maaskofu Eritrea iliyochapishwa hivi karibuni, inayogusia kwa namna ya pekee: maadhimisho ya Mwaka wa Imani na umuhimu wake katika maisha ya waamini; hali hali wanayokabiliana nayo wananchi wa Eritrea katika kipindi hiki; maafa yanayoendelea kutokea kwa wahamiaji wanaozama maji baharini wakitafuta maisha bora zaidi; ubora wa maisha nchini Eritrea. RealAudioMP3

Maaskofu wanachambua hali ya kisaikolojia na kimaadili miongoni mwa wananchi. Katika maisha ya kijamii wanazungumzia kuhusu familia na umuhimu wa kuboresha maadili, utawala wa sheria, elimu na uchumi. Maaskofu wanapembua hali ya maisha ya kiroho na kimaadili miongoni mwa wananchi wa Eritrea kwa kugusia mzizi wa dhambi na hatimaye umuhimu wa kuanza mchakato wa ujenzi wa misingi ya amani na utulivu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Eritrea likisukumzwa na imani limeamua kuwaandikia waamini na watu wote wenye mapenzi mema barua ya kichungaji inayowachangamotisha kusimama kidete kujenga umoja, urafiki na mshikamano wa karibu zaidi na Yesu Kristo kwa kuongozwa na changamoto zilizotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI katika Waraka wake wa Kichungaji, Mlango wa Imani, “Porta Fidei”, ili waamini wote waweze kuimarika katika imani kwa Kristo na Kanisa lake pamoja na kuendelea kuwatangazia watu Injili ya Furaha kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko, kwani kuna furaha kubwa katika imani.

Maaskofu wanaainisha maana ya imani, umuhimu wake katika maisha ya waamini pamoja na kuhakikisha kwamba, imani hii haibaki inaelea katika ombwe bali inamwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu, ili kuwajengea watu matumaini, kwani Yesu Kristo ndiye njia, ukweli na uzima. Kwa njia ya imani, watu wanaweza kudumisha utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; wanaweza kuguswa na mahangaiko ya jirani zao ili kuonesha moyo wa upendo na mshikamano wa dhati, ili kwa pamoja waweze kuonja furaha ya uzima wa milele.

Wananchi wa Eritrea kimsingi ni watu wenye imani thabiti, wanaotambua tofauti zao kama utajiri na kwamba, hawa ni watu wenye kiu ya amani ya kudumu, ndiyo maana Maaskofu wanauliza, Je, ndugu yako yuko wapi? Maaskofu wanatambua kinzani na migogoro iliyojitokeza nchini mwao na umuhimu wa kutibu madonda haya ya utengano kwa kufanya toba na wongofu wa ndani, ili kuwa watu wapya katika maisha ya kiroho, kimaadili na kihadhara.

Kwa masikitiko makubwa Maaskofu wa Eritrea wanasema kuna biashara haramu ya binadamu inayoendelea kutesa na kuwanyanyasa watu kwa kuwajengea matumaini yasiyokuwa kweli na matokeo yake, kuna maelfu ya watu wanaokufa kwa baridi, njaa, kiu na utupu jangwani na wale wachache wanaobahatika kuvuka jangwa, wanakufa maji baharini. Eritrea inawalilia watoto wake wote waliokufa wakiwa njiani kutafuta maisha bora ughaibuni. Bado kuna makundi makubwa ya watu wanaoikimbia Eritrea. Kila mtu anapaswa kuwwajibika kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya jirani yake nchini Eritrea wanasema Maaskofu.

Je, hakuna uwezekano wa kuboresha hali ya maisha ya wananchi wa Eritrea wakiwa nchini mwao? Je, Eritrea inaweza kuwa na amani ya kweli inayohamasisha Injili ya uhai dhidi ya utamaduni wa kifo? Tatizo la wananchi wa Eritrea kukimbilia ughaibuni limeendelea kupigwa dana dana na Jumuiya ya Kimataifa, kumbe, umefika wakati kwa wananchi wa Eritrea kujipanga wenyewe na hatimaye, kuibua mbinu mkakati wa maendeleo, kwani huko ambako vijana wanakimbilia, kunawaka moto! Watu wanakufa maji bila utani!

Wananchi wengi wa Eritrea wanasema Maaskofu wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha kutokana na magonjwa, njaa na umaskini mambo yanayowapelekea hata wakati mwingine kukimbilia uhamishoni wakidhani kwamba, huko pengine wanaweza kupata nafuu ya maisha. Matokeo yake Eritrea inaendelea kupoteza rasilimali watu na wataalam ambao hawatarudi tena, kwani wengi wao wanakufa maji baharini, wale wanaobahatika kufika kwenye Nchi ya ahadi, kamwe hawatarudi tena Eritrea!

Wananchi wengi wa Eritrea hawana uhakika wa usalama na ubora wa maisha yao kwa siku za usoni, ni watu wanaoteseka kisaikolojia na kimaadili, kiasi cha kukata tamaa ya maisha. Kuna idadi kubwa ya wazee ambao hawana tena msaada kutoka katika familia zao kwani wameachwa pweke, hali inayochangia kuzorota kwa uchumi na huduma; watu wengi wanakabiliana na magonjwa ya kisukari, msongo wa mawazo na magonjwa ya moyo! Kwa uchungu mkubwa Maaskofu wanasema, hapa kuna mmong’onyoko mkubwa wa maadili na utu wema.

Maaskofu wanapenda kuwahimiza wanafamilia kutekeleza dhamana na wajibu wao kikamilifu licha ya matatizo na changamoto zilizopo nchini Eritrea, kwani familia bora ni msingi wa maendeleo endelevu ya watu, chemchemi ya imani na hekima, kumbe, kuna haja ya kuimaarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Umefika wakati kwa viongozi na wananchi wote wa Eritrea kujikita katika toba na wongofu wa ndani kwa kuchuchumilia: utu na heshima ya binadamu; haki msingi na mafao ya wengi kwa kuondokana na ubinafsi, rushwa na ufisadi; ubaguzi na upendeleo. Watu wajenge tabia ya ukweli na uwazi, uwajibikaji pamoja na uchaji wa Mungu, ili kupambana fika na ukiukwaji wa sheria unaopelekea kutoweka kwa amani na utulivu. Wanasiasa waoneshe ukomavu katika masuala ya kisiasa kwa kukazia ukweli, uwajibikaji na utawala wa sheria.

Vyombo vya sheria vitekeleze dhamana yake bila upendeleo wala vitisho kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi. Wanasiasa wakuze na kuimarisha utamaduni wa kujadiliana, kusikilizana na kutafuta ukweli kwa pamoja hata katika tofauti zao. Vijana wajengewe uwezo wa kupambana na maisha yao kwa njia ya elimu makini inayojikita katika maendeleo ya sayansi na teknolojia na kwamba, Kanisa litaendelea kushirikisha utajiri, uzoefu na mang’amuzi yake katika sekta ya elimu nchini Eritrea.

Uchumi wa nchi hauwezi kuendelea kutegemea msaada unaotumwa na wananchi wa Eritrea wanaoishi ughaibuni, bali kuna haja ya kufufua mikakati na sera makini za uchumi kwa kuboresha tija na uzalishaji katika sekta ya kilimo, viwanda na huduma pamoja na kuhakikisha kwamba, walau kuna fursa za ajira ili kuongeza pato ya wananchi kuweza kuwa na nguvu ya manunuzi.

Maaskofu wanawaalika waamini na wananchi wa Eritrea katika ujumla wao kufanya toba na wongofu wa ndani, ili kuboresha maisha yao ya kiroho na kimaadili; kwa kukuza dhamiri nyofu na uchaji wa Mungu. Kwa njia hii, watu wanaweza kumwogopa Mwenyezi Mungu na kuwajali jirani zao! Vinginevyo, biashara ya binadamu na viungo vyake itaendelea kushamiri; ngono na utumwa mamboleo yatakuwa ni mambo ya kawaida; uchu wa mali na madaraka yatakuwa ni mapambo ya wengi na matokeo yake ni kuanguka kwa taifa!

Baraza la Maaskofu Katoliki Eritrea linahitimisha barua yake ya kichungaji kwa kuwataka watu wajifunze kuikimbia dhambi na nafasi zake; wajikite katika hija ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa ili kuponya madonda ya utengano, uchoyo na ubinafsi.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.