2014-06-09 08:57:06

Mikakati ya maendeleo kwa Misri!


Bwana Abdel-Fattah el-Sissi, mwenye umri wa miaka 59, Jumapili tarehe 8 Juni 2014 ameapishwa rasmi kuwa Rais wa Misri baada ya kuibuka kidedea katika kinyang'anyiro cha uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Misri hivi karibuni. Katika hotuba yake amekazia umuhimu wa wananchi wa Misri kushiriki kikamilifu katika mchakato wa upatanisho wa kitaifa, ili kuponya madonda ya chuki na utengano kwa kukazia utawala wa sheria.

Anasema, atalivalia njuga tatizo la rushwa na ufisadi nchini Misri, ataendelea kukazia uhuru, haki jamii na utengenezaji wa fursa za ajira, ili watu waweze kujipatia riziki yao pamoja na kukuza utamaduni wa kusikilizana kama sehemu ya mafao ya wengi, ustawi na maendeleo ya Misri.

Katika utawala wake, Misri inapenda kujielekeza zaidi katika ukuzaji wa haki na utulivu katika Ukanda wa Nchi za Kiarabu kwa kuwataka wananchi wa Misri kufanya kazi kwa juhudi na maarifa ili kukuza na kudumisha haki, uhuru na umoja wa kitaifa.

Rais El-Sissi anakuwa ni Rais wa nane kuingia madarakani tangu kulipotokea mapinduzi ya kijeshi kunako mwaka 1953. Kwa miaka mingi Misri imeongozwa na Marais wanaotoka jeshini, isipokuwa Rais Morsi aliyeng'olewa madarakani na Marais wengine ambao walikuwa ni raia walioongoza katika kipindi cha mpito!







All the contents on this site are copyrighted ©.