2014-06-09 09:12:52

Marais Shimon Peres na Abbas Mahmoud waungana na Papa kuomba amani


Jumapili 08 June 2014, majira ya Alasiri, ulikuwa ni wakati nadra wa kihistoria , ndani ya Bustani za Vatican, ambako kulifanyika mkutano wa sala kwa ajili ya kuombea amani. Rais Shimon Peres wa Israel na Rais Mahmoud Abbas wa Palestina, waliketi pamoja karibu karibu, wakiitikia mwaliko wa Papa Francisko, alioutoa wakati akifanya hija katika Nchi Takatifu mwezi jana. Sala hii ilifanyika mbele ya Patriaki wa Constantinople, Bartholomayo I na Msimamizi wa Maeneo Matakatifu katika Nchi Takatifu Padre Pizzaballa, wakiwepo pia wageni wengine waalikwa. Sala zilitolewa katika lugha mbalimbali, lakini zote zikilenga katika nia hiyo ya kuomba amani kwa Mashariki ya Kati na dunia kwa ujumla . Baadaye Hotuba ya Papa Francisko, ilifuatiwa na hotuba za Marais hao wawili na mkutano binafsi.

Taarifa zinasema, wakati huo , ulikuwa ni wakati wa kusisimua kwa viongozi hao watatu, ambao walikumbatiana kwa moyo wa udugu na upendo , wakimtolea Mungu muumbaji shukurani , kuomba msamaha, na kuombea amani. Amani kati ya watu, Wayahudi, Wakristo na Waislamu na amani katika Nchi Takatifu, ni msisitizo ulitolewa na Papa na Marais hao wawili katika hotuba zao.

Papa Francisko , alionyesha tumaini kubwa kwamba, kukutana ana kwa ana kwa Marais hao, itakuwa ni mwanzo wa njia ya kutafuta mikakati mipya ya kuwaunganisha na kuondokana na mgawanyiko wa siku nyingi. Papa akiongoza maombi ya watu wengi wenye mapenzi mema waliokuwa wamefikla katika bustani hizo wa dini, tamaduni na mataifa mbalimbali, aliomba, ili kwamba, atoe jibu kwa hamu ya wakereketwa wote, wanao tamani amani na kuwa na ndoto ya dunia ambayo wanaume na wanawake wanaweza kuishi kama ndugu na si kama wapinzani au maadui.

Papa aliwakumbusha kwamba, dunia ni urithi tulioupokea kutoka kwa mababu zetu. Na pia ni kweli tu kwamba, ni dhamana tuliyokabidhiwa kwa ajili ya watoto wetu: wana ambao wamechoshwa na kudhoofishwa na migogoro na sasa wana hamu ya kuona mapambazuko mapya ya amani. Wana wanaotutaka tuvunje kuta za uadui na kuchukua njia ya mazungumzo na amani kwa upendo na ushindi wa urafiki .

Papa Francisko aliendelea katika hotuba yake kuwakumbuka pia wale wote waliopoteza maisha yao katika vurugu na vita, ili kwamba sadaka ya maisha yao isipotee bure. Na hivyo aliwaomba wageni wake, Peres na Abbas, kuwa na ujasiri wa amani, wa kudumu katika mazungumzo kwa gharama zote, na kuwa na subira katika michakato thabiti lakini yenye kufanyika kwa amani, kuheshimiana na mshikamano.

Papa aliasa kutengeneza amani kunahitaji ujasiri, kuliko vita. Kunahitajika ujasiri wa kusema ndiyo katika , kuketi kwenye mikutano na si mapambano; ndiyo katika mazungumzo na si vurugu; ndiyo katika kukataa mazungumzo yenye kujenga uadui na machukizo. Ni kusema ndiyo katika kuheshimiana , na hapana katika kuwa wanafiki. Kwa haya yote, kunahitajika ujasiri, ujasiri mkubwa. Papa alisisitiza.
Ili kuweza kuifikia amani hiyo , kunahitajika msaada wa Mungu . Papa alieleza na kwa kurejea historia ambayo inatufundisha kwamba nguvu ya vikosi vya binadamu peke yake haitoshi kufanikisha amani. Hivyo kuna haja ya kuinua macho yetu yote mbinguni na kwa utambuzi kwamba, sisi sote tu watoto wa Baba mmoja. Papa alifunga hotuba na sala ya kuomba msaada wa maombezi ya Mama Bikira Maria , na neno 'amani, shalom, salam',liwe neno la siku zote katika maisha yetu.








All the contents on this site are copyrighted ©.