2014-06-07 15:12:07

Uhuru wa kidini!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 7 Juni 2014 amekutana na kuzungumza na Rais Enrique Pèna Nieto wa Mexico na baadaye pamoja na ujumbe wake wamekutana na kuzungumza na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Katika mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu na Rais wa Mexico, kwa pamoja wamegusia hali ya maisha nchini Mexico pamoja na kuangalia mabadiliko mbali mbali yaliyofanywa nchini humo hususan katika Katiba ya Nchi inayojadili kwa namna ya pekee uhuru wa kidini. Viongozi hawa wawili wamezungumzia pia masuala mbali mbali kama vile uhamiaji, mapambano dhidi ya baa la umaskini, ukosefu wa fursa za ajira pamoja na mikakati ya kupambana na biashara haramu ya dawa za kulevya.

Mwishoni, Baba Mtakatifu na mgeni wake, wamebadilishana mawazo kuhusu masuala ya kitaifa na kimataifa!







All the contents on this site are copyrighted ©.