2014-06-07 07:13:55

Peleka Roho wako na sura ya Nchi itageuka!


Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika ujumbe wake kwa Siku kuu ya Pentekoste kwa Mwaka 2014, linawatakia waamini na watu wote wenye mapenzi mema, upendo na amani inayobubujika kutoka kwa Yesu Kristo. Kuna mengi yanayoapswa kuadhimishwa kwa kushikamana kwa pamoja, ili kuleta mageuzi katika kazi ya uumbaji, kwa kutoa nafasi kwa Roho Mtakatifu ili aweze kuumba tena sura ya nchi kutokana na wasi wasi na mashaka yanayoendelea kujidhihirisha katika ulimwengu mamboleo.

Mazingira yanapaswa kufanyiwa marekebisho makubwa kwa ajili ya mafao ya wengi, kwani kuna uhusiano wa karibu kati ya uharibifu wa mazingira na madhara yanayojitokeza katika maisha ya binadamu na jamii inayomzunguka na kwamba, kwa sasa maisha ya mwanadamu yako hatarini pengine kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya binadamu!

Lengo la Pentekoste kadiri ya mpango wa Mungu ni kuleta umoja na mshikamano kutokana na mgawanyiko wa watu katika sura ya dunia uliosababishwa na kuvurgika kwa lugha. Utekelezaji wa ahadi hii ya Mungu inaonesha kana kwamba, inakinzana na uhai wa binadamu katika nyakati hizi. Lakini ikumbukwe kuwa uwepo wa Mungu katika maisha ya mwanadamu ni chemchemi ya utakatifu, maendeleo na utambulisho wake, mambo ambayo kwa sasa yako hatarini.

Kwa njia ya Pentekoste, ukweli kuhusu uumbaji unajionesha kwa namna ya pekee katika sala ambayo inamwonesha Mungu kuwa kweli ni Mungu wa Uhai anayependa kuwaelekeza watu katika haki na amani. Baraza la Makanisa linamwomba Roho Mtakatifu aweze kuwashukia, kujidhihirisha kati yao na kuwawezesha kuwa wamoja!








All the contents on this site are copyrighted ©.