2014-06-07 12:07:11

Boko Haram inalidhalilisha Jeshi!


Kardinali John Onaiyekan wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria anasema kwamba, vitendo vya kigaidi vinavyoendeshwa na Kikundi cha Boko Haram bila kudhibitiwa kwa kuhofia kwamba, kwa kupambana na Boko Haram kuna maanisha kupambana na waamini wa dini ya Kiislam ni kuwa na tafsiri finyu ya ukweli wa mambo. Hakuna upinzani kati ya Wakristo na Waisla, vyombo vya ulinzi na usalama havina budi kukishughulikia Kikundi cha Boko Haram kama kikundi cha kigaidi na wala si dhehebu la dini ya Kiislam!

Mahakama ya Kijeshi nchini Nigeria imewatia hatiani baadhi ya viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama ambao wamekuwa wanajihusisha na uuzaji wa silaha za moto kwa Boko Haram, ingawa taarifa hizi zimekanushwa na Kamanda mkuu wa Jeshi la Nigeria anasema Kardinali Onaiyekan. Lakini ana uhakika kwamba, iko siku wananchi wa Nigeria watafahamu ukweli wa mambo na wapi Boko Haram wanapata silaha za kufanya mashambulizi kiasi cha kutetekeza kijiji kizima. Kama habari hizi ni za kweli, basi wanajeshi wenye uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka wanalichafua jeshi na ndiyo maana Serikali inashindwa kuwathibiti kutokana na vitendo vinavyoendelea kusababisha madhara makubwa kwa usalama wa watu na mali zao!

Kardinali Onaiyekan anasema, Boko Haram si vita kati ya Wakristo na Waislam na wale wanaotazama tatizo hili katika mwelekeo kama huu wanakosema. Boko Haram ni kikundi cha kigaidi, kinachopaswa kushughulikiwa kadiri ya sheria za nchi ya Nigeria pamoja na sheria za kimataifa. Vyombo vya ulinzi na usalama vinaundwa na waamini wa dini mbali mbali, kumbe, ikiwa kama udini unatumika kwa ajili ya kuwakingia kifua Boko Haram hapa ni hatari kubwa na ukiukwaji wa maadili na kanuni za Kijeshi na kwamba, wahusika wanapaswa kushughulikiwa kikamilifu!

Boko Haram licha ya mikakati inayoendeshwa na Nigeria kwa kusaidiana na Jumuiya ya Kimataifa, lakini bado linafanya mashambulizi kwa watu wasiokuwa na hatia. Wasichana wa shule waliotekwa nyara hivi karibuni bado hawajaachiliwa huru, hii inaonesha kwamba, Serikali inashindwa kutawala baadhi ya maeneo ya ardhi yake, jambo ambalo linatia shaka sana.

Kuna haja kwa Nigeria kufanya majadiliano ya kina katika ukweli na uwazi ili kuamua mustakabali wa Nigeria kwa sasa na kwa siku za baadaye. Mikakati ya kijeshi peke yake haitoshi, kumbe kuna haja ya kuwa na sera na mikakati mipana zaidi kwa kushugulikia pia tatizo la rushwa na ufisadi, mambo ambayo pengine yanagumisha mapambano dhidi ya Kikundi cha kigaidi cha Boko Haram.







All the contents on this site are copyrighted ©.