Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake, Ijumaa tarehe 6 Juni 2014 kwenye Kikanisa
cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican amewataka Mapadre na Watawa kuonesha
upendo wa pekee kwa Yesu Kristo kabla hata ya mambo mengine yote kama vile masomo
ya falsafa na taalimungu na kwamba, wanatumwa na Kristo kuchunga kondoo wake.
Huduma
ya uchungaji inafumbata utajiri wote ambao Mapadre na Watawa wamejichotea kutoka katika
falsafa, taalimungu na mafundisho ya Mababa wa Kanisa, kumbe jambo la pili ni Mapadre
kuhakikisha kwamba, wanakuwa ni wachungaji, wema, wachapakazi na watakatifu, kwani
wameitwa na kuwekwa wakfu kwa ajili ya kuwachunga Watu wa Mungu na wala si vinginevyo!
Baba Mtakatifu anawaombea Makleri neema ya kuendelea kutambua upendo wao kwa
Kristo na Kanisa lake, ili waweze kujisadaka kwa ajili ya Familia ya Mungu wanayoihudumia,
wakiwa tayari kujifunza na kufuata nyayo za Yesu Kristo.