2014-06-06 08:28:02

Pentekoste


Ni siku nyingine tena tunapokutana katika meza ya Neno la Mungu. Leo tunaadhimisha sherehe ya Pentekoste, sherehe ambayo katika kalenda ya litrujia huja siku hamsini baada ya pasaka. RealAudioMP3

Ni sherehe ambayo wakristu humshangilia Kristu mfufuka katika Roho Mtakatifu na kufurahia ukombozi ambao umeletwa na Kristo mwenyewe. Katika sherehe ya Pentekoste fumbo la pasaka hukamilika maana ni katika sikukuu hii Roho Mtakatifu hulishukia Kanisa ili likaendeleze kazi ya Kristu bila woga, likiwa na nguvu za kimungu. Ni sherehe ambayo kwayo Roho Mtakatifu huthibitisha muungano wetu na Mungu. Ujumbe wa Neno la Mungu unalala katika Roho Mtakatifu kuwa sheria mpya na nguvu ya Wakristu, taifa jipya lililoshikamana katika upendo na Mungu.

Katika somo la kwanza toka kitabu cha Matendo ya Mitume, tunaona Mitume wakiwa mahali pamoja na ghafla upepo na uvumi, ndimi za moto zinawashukia. Wote wakajazwa na Roho Mtakatifu na kuanza kunena kwa lugha mbalimbali. Wanapokea nguvu ya Mungu na hivi wanaweza kutenda matendo ya ajabu kwa mataifa.

Tunasikia pia, watu waliwashangaa Mitume kwa kuwa watu hawa waliweza kusikia na kuelewa ujumbe uliokuwa ukihubiriwa na Mitume katika lugha zao. Hii ni ajabu maana baada ya mnara wa Babeli (Mw.11:1-9) watu hawakuweza kuelewana kiurahisi. Kumbe Roho Mtakatifu ni muunganishi wa taifa jipya la Mungu ambalo ni tunda la ufufuko.

Ishara mbalimbali tulizozisikia hapo juu zatupa mwanga ili kuweza kuelewa vema tendo la kushuka kwa Roho Mtakatifu. Uvumi wa upepo na ndimi za moto zinatupa mazingira ya sheria ya zamani, yaani wakati sheria ya zamani ilipokuwa ikitangazwa tunaposoma katika kitabu cha Kutoka, kulitokea alama hizo (Kut.19:16).

Wakati Musa alipokuwa akipokea sheria ya Mungu maneno ya Mungu yalibadilika na kueleweka katika ndimi sabini za moto (Kut.20:18). Hili lilimaanisha kuwa sheria hii ni kwa ajili ya watu wote duniani. Luka anapoandika jambo la kushuka kwa Roho Mtakatifu anatumia alama zilezile ili aweze kueleweka kwa urahisi kwa walengwa wa Neno la Mungu.

Mwinjili Luka anatumia alama ya lugha nyingi akionesha utamaduni uliokwishajengeka katika Kanisa la mwanzo, yaani watu walipompokea Roho Mtakatifu walinena kwa maneno mapya wakimsifu Mungu. Alama hii ni kielelezo cha umoja wa Kanisa, yaani Kanisa lililo kwa ajili ya wokovu wa wote. Injili ni kwa ajili ya mataifa yote, inatupilia mbali mipaka ya rangi, kijiografia, lugha na mambo yote yaletayo hatari na kuvuruga umoja wa taifa la Mungu.

Ni kwa njia ya Pentekoste wale wote waliotawanyika wanakusanywa tena kwa sheria mpya yaani, sheria ya mapendo inayounda familia mpya ya Mungu. Sheria hii inaandikwa mioyoni mwa watu.

Mtakatifu Paulo anapowaandikia Wakorinto anawakumbusha kuwa karama walizopewa si kwa ajili ya ubinafsi bali kwa ajili ya umoja. Anawaambia kuwa Roho ni mmoja na karama ni mbalimbali kwa ajili ya shughuli za misioni, kwa ajili ya kupamba upendo uleule. Anawakumbusha hilo akitumia alama ya mwili mmoja ulio na viungo mbalimbali vyenye shughuli mbalimbali kwa ajili ya mwili huo mmoja. Mwishoni anataka karama ziwe ni chanzo cha mapendo katika familia yao ndiyo Kanisa.

Hivi leo katika jamii mbalimbali kuna machafuko kwa sababu ya kila mmoja kuona karama aliyonayo ni kwa ajili yake mwenyewe na si kwa ajili ya jumuiya yake. Yafaa kuepuka shida hii mapema ili jumuiya yetu ikae kwa amani.

Katika injili mwinjili Yohane anatangaza amani ya Kristu ambayo ni zawadi ya ufufuko na ni msingi wa umisionari. Si tu msingi wa umisionari bali pia ni msingi wa upatanisho na furaha katika familia ya Mungu maana baada ya kuwapatieni amani atawatuma ulimwenguni kwa ajili ya kazi ya kitume. Katika utume, Mitume wanaalikwa kuwaondolea watu dhambi zao.

Hawewezi kuondolea dhambi bila Roho wa Mungu na hivi kabla anawavuvia Roho huyo. Kumbe mpendwa kushuka kwa Roho Mtakatifu ni nguvu ya ondoleo la dhambi ni amani na furaha ya taifa la Mungu, ni mkazo wa umisionari kazi ya Kristu.

Roho Mtakatifu anashuka kwa ajili ya kubadili maisha yetu yawe maisha mapya, yawe ni maisha kwa ajili ya kuwafariji walio katika taabu mbalimbali. Basi ni wajibu wetu sisi tuliompokea kwa njia ya sakramenti kuweka maisha yetu kama kielelezo cha maisha mapya, maisha yampendezayo Mungu na watu. Tukishampokea Roho Mtakatifu hatutaweza tena kuangalia mambo ya chini bali yaliyo ya juu. Ndiyo kusema Roho wa Bwana akishaujaza ulimwengu huunganisha viumbe vyote kwa ajili ya umoja kamili na Mungu.

Mpendwa katika siku ya leo tuliombee Kanisa ili liwe kielelezo cha amani na upendo na mshikamano. Tuwaombee wote waliojiweka wakfu katika Roho Mtakatifu wakatimize kazi yao ya wakfu kwa furaha na amani. Ninakutakieni sherehe njema na mwendelezo mzuri wa maisha ya furaha. Ninakukumbusha kuwa leo Mama Kanisa anahitimisha kipindi cha Pasaka. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.