2014-06-04 06:52:56

Mfumo dume unavyokwamisha mapambano dhidi ya Ukimwi


Imeelezwa kuwa mikakati ya Serikali ya Tanzania katika kupambana na kuondoa mfumo dume bado unakumbwa na vikwazo kutokana na mfumo huo kuhamia katika mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya ukimwi na ukimwi. Taarifa hiyo imesema wanaume walio wengi mkoani Mbeya wanawatumia wake zao kama 'sample' ya majibu ya kufahamu afya zao baada ya kuwatuma kwenda kupima peke yao katika vituo vya upimaji wa hiari, zahanati, vituo vya afya na hospitalini.


Hayo yamesemwa na Mnasihi wa ushauri nasaha kuhusu mapambano ya virusi vya ukimwi na ukimwi, Shirika la misaada ya Kanisa Katoliki Caritas Mbeya, kituo cha Iyunga, jijini Mbeya, Alex Kumwenda wakati akitoa taarifa katika kikao cha mpango kazi cha kila mwisho wa mwezi. Bwana Alex ametoa ushauri kwa wafanyakazi kuwa wa kwanza kuonesha mfano kwa jamii ili nao waweze kuiga na kwamba tatizo hilo limeingia hadi katika masuala ya uzazi ambapo wanaume licha ya kushauriwa kuwasindikiza wenzi wao bado wanakwepa.

Msimamizi wa waelimishaji rika caritas Teddy Haizenje amesema upo umuhimu wa kuwatumia waelimishaji rika katika Kata mbalimbali ili kuelezea umuhimu wa kusindikizana kwa wenza katika kupima afya zao kwa pamoja na madhara ya kupima na kuamini usalama kwa majibu mwanaume au mwanamke.


Naye Ofisa ugani wa Caritas Parokia ya Igurusi, wilayani Mbarali, Luckson Mwakilindile ameshauri kufanyika kwa kampeni maalum ya kuielimisha jamii faida ya kushiriki kwa pamoja kupata majibu ya afya zao ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza baada ya kupokea majibu kwa upande mmoja ikiwemo kuandaa matamasha,semina na makongamano kwa kushirikiana na wafadhiri mbalimbali.

Hata hivyo Mkurugenzi wa Idara ya caritas na maendeleo Jimbo katoliki la Mbeya, Edgar Mangasila amesema kutoa ripoti haitoshi na kwamba kama shirika wanapaswa kushirikiana na jamii wanayofanya nayo kazi katika kuielimisha na kuihamasisha umuhimu wa mume na mke kwenda kwa pamoja kupima kwa hiari.

"Ili ni jukumu letu sote na tulione hili ni tatizo,hivyo tunapaswwa kwa umoja wetu kila mmoja katika mahali pake pa kazi ashirikiane na jamii husika kutoa elimu na kuhamasisha umuhimu wa kwenda pamoja kupima kwa hiari afya....hii ya kutoa tu ripoti haitoshi lazima tubebe utajiri wa kuhakikisha tunapata ufumbuzi wa kutatua tatizo hili katika jamii yetu,"amesema mangasila.

Ameongeza Mkurugenzi huyo,"mabwana shamba lazima muwashirikishe wakulima huko mnakofanya nao kazi, wasimamizi wa masuala ya wanawake,jinsia na watoto nanyi kw anafasi yenu huko mlipo,wahasibu,waratibu sote tunawiwa na jamii hii kuiokoa na kuondoa magumu na makando kando yanayojitokeza."

Kikao cha mpango kazi katika Idara ya Caritas Jimbo Katoliki la Mbeya kinafanyika kila mwisho wa mwezi ambapo wafanyakazi wanaanza kwa kukutana kwa idara husika katika kikao cha awali kufanya mang'amuzi ya utume wao ambapo siku inayofuata wanakutana katika vitengo vyote kutoa taarifa za kazi zilizofanyika kwa mwezi husika na mpango kazi wa mwezi unaofuata.

Katika kikao hicho pia alitambulishwa mfanyakazi wa kujitolea kutoka nchini Italia, Chiara Cantoni anayefanya kazi na Mbeya Community Based rehabilitation program for Children with Disabilities (Mbeya CBR- Simama) wanaoshirikiana na Caritas Jimbo la Mbeya.

Chiara naye alitoa ripoti kutoka CBR-Simama ambapo alishukuru kwa moyo wa upendo na ushirikiano alioukuta kwa wafanyakazi wa Caritas na ameahidi kushirikiana kwa pamoja kwa hatua zote.

Na Thompson Mpanji,
Mbeya, Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.