2014-06-04 11:28:29

Ebo! Upadre si ujiko!


Upadre ni wito wa huduma unaotoa nafasi kwa Padre kumkumbatia Yesu moyoni mwake, tayari kumpeleka kwa wengine katika ari na moyo mkuu, bila ya kujibakiza katika huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Upadre si ujiko wala kazi!

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko aliyowaandikia majandokasisi wanaojiandaa kuwa Mapadre kutoka Cuba waliomwomba ushauri katika safari ya majiundo yao katika maisha na wito wa kipadre. Baba Mtakatifu amewashukuru majandokasisi hawa kwa barua yao na anawataka kusonga mbele kwa moyo mkuu pasi na kukata tamaa katika maisha na wito wao wa Kipadre, ili hatimaye, siku moja waweze kuwa kweli ni Mapadre, wema na watakatifu wanaojisadaka kwa ajili ya huduma kwa Familia ya Mungu nchini Cuba.

Baba Mtakatifu anawataka majandokasisi hawa wanaosoma katika Seminari ya Mtakatifu Basil Mkuu Santiago di Cuba kujizatiti kweli kweli kwani inalipa kudumu hadi mwisho katika maisha na wito wa Kipadre. Baba Mtakatifu anawataka Majandokasisi hawa kuonesha unyenyekevu na kupokea kwa ukarimu: ushauri, mafunzo na majiundo yanayotolewa kwao na walezi wao.

Waseminari wakubali kufundwa kiakili, kiroho, kimaadili, kiutu na katika mikakati ya shughuli za kichungaji, wakikazia maisha ya kijumuiya ili kujenga na kuimarisha udugu na mshikamano wa kipadre!







All the contents on this site are copyrighted ©.