2014-06-03 08:27:09

Mkutano wa viongozi wa kidini kuhusu mikakati ya maendeleo endelevu!


Kamati ya ufundi kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madgascar, SECAM, hivi karibuni imemaliza kikao chake cha siku tatu kilichokuwa kinafanyika Jijini Kampala, Uganda kama sehemu ya maandalizi ya mkutano wa viongozi wa dini kuhusu maendeleo endelevu baada ya mwaka 2015 unaotarajiwa kufanyika mjini Entebbe, Uganda, kati ya tarehe 1- 2 Julai 2014. RealAudioMP3

Mkutano wa maendeleo endelevu huko Entebbe unapania pamoja na mambo mengine kuendeleza mchakato wa mikakati ya Maendeleo ya Millenia baada ya Mwaka 2015, iliyokuwa imebuniwa na Umoja wa Mataifa. Huu utakuwa ni mkutano wa kujadili mikakati ya maendeleo na matokeo yake na kwa namna ya pekee, itakuwa ni fursa ya kuweza kuwashirikisha viongozi wa kidini kutoka Barani Afrika.

Lengo ni kusaidia kuwahamasisha viongozi wa Serikali na taasisi katika nchi zao kuhusu sera na mikakati inayopania kuendeleza uchumi unaozingatia masuala msingi katika maisha ya kijamii; ushirikishwaji wa jamii na upatanisho. Mambo mengine ni kuendelea kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu pamoja na kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi.

Mkutano wa viongozi wa kidini Barani Afrika utawahusisha viongozi wa dini ya Kiislam, Kikristo pamoja na dini mbali mbali zinazopatikana Barani Afrika. Kamati ya ufundi kutoka SECAM imekutana na kuzungumza na Baraza la majadiliano ya kidini nchini Uganda pamoja na viongozi wa Serikali ya Uganda ili kujadili kuhusu ushiriki wao pamoja na msaada wa kufanikisha mkutano wa viongozi wa kidini kutoka Barani Afrika.








All the contents on this site are copyrighted ©.