2014-06-03 11:33:57

Kimbilieni huruma na upendo wa Mungu kwani mnaye Mwombezi!


Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kukimbilia kwenye kiti cha huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na kifani mara tu wanapoanguka dhambini kwani kuna Mwombezi ambaye daima yuko mbele ya Mwenyezi Mungu kuwaombea na kuwatetea, huyu si mwingine bali ni Yesu Kristo Mkombozi wa dunia! Baba Mtakatifu ameyasema haya wakati wa mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican, Jumanne tarehe 3 Juni 2014, Kanisa linapoadhimisha Kumbu kumbu ya Mashahidi wa Uganda.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu si tu kwamba, anazungumza na kuwatetea mbele ya Baba yake wa mbinguni, lakini zaidi anawapenda na amegharimia ukombozi wa binadamu kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake. Madonda matakatifu ya Yesu ni kielelezo cha huruma na upendo wa Mungu kwa wakosefu. Yesu baada ya ufufuko wake na kupaa kwenda mbinguni kwa Baba yake ameendelea kuyatunza mwilini mwake Madonda Matakatifu, ili yaweze kuwa ni alama ya kuwaombea huruma na msamaha mbele ya Mwenyezi Mungu.

Madonda Matakatifu ya Yesu ni matokeo ya dhambi za binadamu, chachu ya huruma na upendo wa Mungu ili kuweza kuwaimarisha wafuasi wake katika imani na matumaini kama ambavyo Yesu mwenyewe alimwombea Mtakatifu Petro ili akiishakuimarika katika imani aweze pia kuwaimarisha ndugu zake katika imani kwa Kristo na Kanisa lake!







All the contents on this site are copyrighted ©.