2014-06-02 12:06:48

Upendo unajikita katika uaminifu, udumifu na kuzaa matunda!


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican, Siku ya Jumatatu tarehe 2 Juni 2014 amesema kwamba, upendo unaorutubisha maisha ya Kanisa kutoka kwa Kristo mwenyewe unajikita katika uaminifu, udumifu na unaozaa matunda!

katika Ibada hii kulikuwepo na wanandoa waliokuwa wanaadhimisha kumbu kumbu ya miaka 25, miaka 50 na miaka 60 tangu walipofunga Sakramenti ya Ndoa Kanisani na kwamba, walipenda kumshukuru Mungu wakiwa wameungana na Baba Mtakatifu Francisko ambaye anaendelea kutoa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa Ndoa na familia. Baba Mtakatifu amewataka wanandoa hawa kuendelea kuwa waaminifu, kwa kudumu katika Sakramenti ya Ndoa na kuendeleza matunda ya Sakramenti hii ambayo ni watoto, zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, Yesu alionesha upendo wa dhati kwa Kanisa lake na kuutolea ushuhuda makini. Uaminifu na upendo wa Kristo kwa Kanisa lake ni mwanga katika Sakramenti ya Ndoa. Yesu kamwe hachoki kuonesha upendo kwa Kanisa lake hata katika nyakati za magumu na majaribio ya maisha. Upendo kati ya wanandoa ujioneshe kwa namna ya pekee katika kusaidiana na kutatua matatizo na changamoto katika umoja na mshikamano, ili kuendelea kuenzi tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Upendo wa Kristo unaliwezesha Kanisa kupata watoto wapya wanaozaliwa kwa maji na Roho Mtakatifu. Hata katika maisha ya ndoa na familia watu wanaweza kukirimia watoto wenye afya nzuri au hata wakati mwingine watoto ambao afya zao si nzuri sana, lakini wote hawa ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Inasikitisha kuona kwamba, kuna watu katika maisha ya ndoa na familia hawapendi kupata watoto, wanaridhika kukaa katika upweke na kubembeleza paka au mbwa. Fainali za ndoa kama hizi anasema Baba Mtakatifu ni uzee usiokuwa na matumaini, uzee unaoelemewa na upweke na mawazo mabaya!







All the contents on this site are copyrighted ©.