Vifo vya akina mama wajawazito na watoto vimepungua Tanzania
Tanzania imefanikiwa kufanikisha lengo la kupunguza vifo vya watoto kama yalivyoainishwa
na Umoja wa Mataifa kwa juhudi za Serikali, familia na jamii kwa ujumla, ikiwa ni
pamoja na msaada mkubwa kutoka kwa Jumuiya ya kimataifa, washirika wa maendeleo, sekta
binafsi na Mashariki binafsi mbalimbali ya kimataifa. Rais Kikwete amesema hayo tarehe
29 Mei,2014 alipotoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano kuhusu afya ya Mama na Mtoto unaofanyika
mjini Toronto, Canada .
Katika jitihada hizo Tanzania imefanikiwa kupunguza
vifo vya watoto wachanga ambapo kuamkia milenia vifo vya watoto vilikuwa 115 kwa 1,000
na vya watoto wachanga chini ya miaka mitano vilikuwa 191 kwa 1,000. Kufikia sasa,
vifo hivyo vya watoto wachanga vimefikia watoto 21 kwa 1,000 na watoto chini ya miaka
mitano vifo vimepungua hadi kufikia 54 kwa 1,000.
Mambo mengine yaliyochangia
katika kufanikisha, ni udhibiti na mapambano dhidi ya malaria na Ukimwi kama ilivoainishwa
katika Malengo ya Milenia, ambalo ni lengo la 6, kuboresha lishe kwa watoto na kuwanyonyesha.
Ni dhahiri pia kwamba Serikali imeweka sera nzuri za Afya na kuboresha huduma za Afya
na Uzazi Tanzania, kuongeza bajeti ya Afya kutoka shilingi 271 bilioni kwa Mwaka 2007
hadi shilingi trillion 1.4 kwa Mwaka 2013.
Katika hili serikali imejenga
Zahanati 1,640, Vituo vya Afya 122 na Hospitali mpya 19. Pamoja na hayo, Hospitali
za Mikoa na Wilaya , pamoja na Hospitali kubwa nchini ya Muhimbili zimeboreshwa. Serikali
pia imepandisha viwango Zahanati na Vituo vya Afya kadhaa ili kuweza kutoa huduma
ya ukunga, kuongeza mafunzo kwa watumishi na pia kuboresha upatikanaji wa dawa na
vifaa muhimu katika Afya.
Rais Kikwete ameuambia mkutano huo uliohudhuriwa
na Waziri Mkuu wa Canada Mhe. Stephen Harper, Malkia Rania wa Yordan na Bibi Melinda
Gates wa Bill and Melinda Gates Foundation kuwa, ataongeza bajeti ya Afya na kwa kushirikiana
na Umoja wa Mataifa, washirika wa Maendeleo, na sekta binafsi na ana matumaini kuwa
malengo haya yanaweza kuendelezwa na kufikiwa zaidi.
Mapema Waziri Mkuu
wa Canada ametangaza msaada wa dola bilioni 3.5 katika kusaidia na kuboresha Afya
ya Mama na Mtoto kwa kipindi cha Miaka 2015-2020 ambapo msaada mkubwa unalenga katika
harakati za kupunguza vifo vya Mama na Mtoto hasa katika kuimarisha mifumo ya Afya,
kuimarisha Lishe na kupunguza magonjwa na kuimarisha chanjo.
Wakati huo
huo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) Bw. Ban Ki Moon amempongeza Rais Kikwete
kwa jitihada zake za kulinda na kuleta Amani DRC Congo "Napenda kutambua na kukushukuru
kwa juhudi zako za kuunga mkono jitihada za Amani na Usalama DRC na kwingineko, natumaini
utaendelea kutoa mchango wako na natazamia mchango wako mkubwa katika nchi za Maziwa
Makuu" Mhe. Ban Ki Moon amemuambia Rais Kikwete ambaye naye ameahidi kutoa ushirikiano
zaidi.