Kardinali George Pell, Mwenyekiti wa Sekretarieti ya uchumi mjini Vatican, akihojiwa
na gazeti moja kutoka Hispania anasema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anaishi maisha
ya kawaida pasi na makuu kama kielelezo cha kumwilisha ufukara katika maisha na utume
wake kiasi kwamba amevunjilia mbali kuta za utengano zilizokuwepo kabla ili kukutana,
kuonana na kuzungumza na watu!
Kardinali Pell anasema, kuna baadhi ya vyombo
vya upashanaji habari ambavyo vinajadili juu juu kuhusu mafundisho tanzu ya Baba Mtakatifu
Francisko katika ulimwengu mamboleo: masuala kama uchu wa mali na madaraka; utamaduni
wa kifo unaokumbatia sera za utoaji mimba; umuhimu wa tunu msingi za maisha ya ndoa
na familia. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, kwa baadhi ya vyombo vya habari kwao
hii si habari inayouzika na matokeo yake wanataka kupindisha habari kuhusu mafundisho
ya kweli ya Papa Francisko, kwa ajili ya mafao yao binafsi.
Hii ni changamoto
kubwa kwa vyombo vya upashanaji habari kujitahidi kuingia katika kiini cha Mafundisho
ya Baba Mtakatifu Francisko, kwa kutambua kwamba, ni kiongozi anayependa kutolea ushuhuda
wa kweli za Kiinjili si tu kwa maneno bali hata katika mtindo wa maisha yake! Ni kiongozi
anayetangaza Injili ya Kristo kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Ni Mtawa aliyefundwa
katika maisha na kanuni za Wayesuit wa zama hizo ndiyo maana anajisadaka bila hata
kujihurumia. Kwake hakuna mapumziko wala kuponda mali! Kazi hadi kieleweke!
Kardinali
Pell anasema kwamba, Baba Mtakatifu katika mikakati ya utekelezaji wa dhamana yake
anakazia umuhimu wa umoja na mshikamano katika kupanga, kuamua na kutekeleza vipaumbele
vya maisha na utume wa Kanisa, ndiyo maana ameamua kuunda Tume ya Makardinali kutoka
sehemu mbali mbali za dunia wanaomsaidia kufanya marekebisho katika Sekretarieti ya
Vatican. Anaendelea kutekeleza changamoto zilizotolewa na Makardinali wakati wa mikutano
yao elekezi kabla ya uchaguzi wa Papa Francisko.
Kardinali George Pell anasema,
Baba Mtakatifu anataka kuona masuala ya ukweli, uwazi, uadilifu na weledi yanafanyiwa
kazi katika huduma mbali mbali zinazotolewa na Kanisa. Sekretarieti ya Uchumi inaundwa
na Makardinali wanane na waamini walei saba, wote wakiwa na kura sawa katika maamuzi
yanayotolewa na Sekretarieti hii.
Hii ni mara ya kwanza katika historia ya
Kanisa kwamba, waamini walei wanakuwa na sauti sawa na Makleri. Baba Mtakatifu bado
anauona umuhimu wa uwepo wa Benki ya Vatican kwa ajili ya kusaidia kuendeleza utume
wa Kanisa sehemu mbali mbali duniani.