2014-05-31 07:36:34

Mshikamano, amani na matumaini kwa Sudan ya Kusini!


Shirikisho la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kimissionari ya Kanisa Katoliki yanayotekeleza utume wake nchini Sudan ya Kusini yamewaandikia waamini na watu wote wenye mapenzi mema ujumbe wa mshikamano, amani na matumaini wananchi wote wa Sudan ya Kusini katika kipindi hiki kigumu cha historia ya nchi yao; kipindi ambacho mtutu wa bunduki unaonekana kutawala zaidi kuliko majadiliano yanayolenga upatikanaji wa amani ya kudumu!

Kuna Mashirika ya Kitawa 29 yanayojikita katika Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili nchini Sudan ya Kusini. Mashirimka haya yanasema yataendelea kuwahudumia wananchi wa Sudan ya Kusini kama sehemu ya utekelezaji wa mchakato wa Uinjilishaji kwa kutoa huduma katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu katika majimbo saba yanayounda Kanisa Katoliki Sudan ya Kusini.

Mashirika haya yanapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati na upendo kwa wananchi wa Sudan ya Kusini kwa kuthamini utu na heshima ya kila mtu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, ili kujenga na kuimarisha: umoja, upendo na mshikamano wa dhati kati ya watu. Wanasikitishwa sana kutokana na vitendo vya umwagaji wa damu ya watu wasiokuwa na hatia vinavyoendelea kwa wakati huu nchini Sudan ya Kusini.

Maelfu ya wananchi wa Sudan ya Kusini wanatamani kuona tena haki, amani, upendo na mshikamano vikitawala miongoni mwao. Watawa wa Mashirika haya wanasema, mawazo yao wanayaelekeza zaidi kwa familia ambazo zimeguswa kwa namna ya pekee na machafuko ya kisiasa nchini Sudan ya Kusini. Wanatambua kwamba, kuna maelfu ya watu ambao wamelazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao; ni watu ambao wamekimbilia msituni au kwenye kambi za wakimbizi za Umoja wa Mataifa.

Wanapenda kuonesha mshikamano wao kwa Makleri na Watawa walionyanyasika kutokana na machafuko haya ambayo yanaendelea kusababisha uharibifu mkubwa kwa miundo mbinu ya nyumba za ibada, shule, hospitali na makazi ya watu. Watawa wa Mashirika haya wanawapongeza wote ambao wameendelea kuonesha mshikamano wa dhati na watu wanaoteseka kutokana na machafuko ya kisiasa pamoja na vita nchini Sudan ya Kusini.

Mashirika ya kitawa na kazi za kitume nchini Sudan ya Kusini yanalaani vita na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia yanayofanywa na Serikali pamoja na wapinzani wake. Kumekuwepo na uvunjifu mkubwa wa haki msingi za binadamu, wizi na uporaji wa mali ya umma na binafsi, lakini katika yote haya wahusika wakuu katika machafuko yanayoendelea Sudan ya Kusini watambue kwamba, utu na heshima ya binadamu ni mambo yanayopaswa kulindwa, kutetewa na kuendelezwa.

Mashirika ya kitawa yanalaani tabia ya rushwa, wizi na ufisadi wa mali ya umma; ukabila; chuki na uhasama; uchu na uroho wa madaraka mambo ambayo yamechangia umwagaji wa damu ya watu wasiokuwa na hatia. Hata katika mazingira ya mauaji na uvunjifu wa haki msingi za binadamu, kuna watu wanaoendelea kutajirika kutokana na uwepo wa biashara haramu ya silaha inayochochea vita na machafuko ya kijamii, hivi ni vitendo vya kinyama ambavyo kamwe haviwezi kufumbiwa macho!

Mashirika ya kitawa na kazi za kitume yanasema kwamba, yataendelea kushirikiana na Kanisa mahalia katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili kwa kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema katika harakati za kuponya madonda ya vita, chuki na kinzani nchini Sudan ya Kusini, ili haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa viweze kutawala tena.

Mwishoni, Mashirika haya yanasema, yataendelea kuwahudumia wananchi wa Sudan ya Kusini kwa ari na moyo mkuu, kwa kujikita katika moyo wa mshikamano, furaha na matumaini kwa ajili ya leo na kesho iliyo bora zaidi kwa wananchi wa Sudan ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.