Ninakuleteni tena tafakari ya Liturujia ya Neno la Mungu, leo tukiwa tunasherehekea
Sikukuu ya KUPAA BWANA MBINGUNI. Sikukuu hii huja siku kumi kabla ya Pentekoste yaani
siku 40 baada ya Ufufuko wa Bwana, wakati Mitume wakimsubiria Roho Mtakatifu.
Baada
ya kazi ya kichungaji na kimisionari hapa duniani Bwana lazima akatoe taarifa kwa
Baba yake wa mbinguni. Kumbe, anapaa mbinguni kwenda pia kutayarisha makao kwa ajili
yetu sote.
Mpendwa msikilizaji, kupaa ni kuingia katika utukufu wa Mungu na
kuachana na kifungo cha kifo. Ni kutenganisha dunia yetu na Mungu na hasa ni kuwa
karibu na Mungu. Aidha Bwana kabla ya kupaa ataweka wazi wajibu kwa Mitume na jumuiya
ya kwanza, akisema “nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.
Basi enendeni
mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba na la Mwana na
la Roho Mtakatifu na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi. Akitambua kwamba
wanahitaji msaada wake daima anawapa tumaini na kuwahakikishia akisema, na tazama
nipo pamoja nanyi siku zote hata ukamilifu wa dahari” Ujumbe huu tunaupata katika
Injili ya Matayo sura ya 28.
Kristo anapopaa anaingia katika utukufu wa Mungu,
ni utukufu ambao hatuwezi kuugusa bali kwa njia ya imani tunaweza kuufikia. Hata hivyo
Bwana kabla ya kupaa katika kipindi cha siku 40 anatoa wosia mbalimbali: Anawaambia
Mitume wasitoke Yerusalemu hadi ahadi ya Baba yake itimie yaani ya kuwapelekea Roho
Mtakatifu atakayewasidia katika utume wao, yaani watatenda na kubatiza katika Roho
Mtakatifu. Anawaambia watapokea Roho wa Mungu na watakuwa mashahidi katika Uyahudi
na Samaria yote. (Mdo 1:8).
Mpendwa ujumbe huu, si kwa ajili ya Mitume tu
bali kwa ajili ya Kanisa zima, ndiyo kusema tuaalikwa kuitikia wosia wa Mungu daima
ambao tunaupata kwa njia ya Neno lake na hasa kuwa mashahidi wa upendo kwa mataifa
kama tulivyosikia Dominika iliyopita.
Mtume Paulo akiwaandikia Waefeso anakazia
imani katika Bwana na anawakumbusha kuwa Kristu ni mfufuka na ni kichwa cha Kanisa
tena ameketi kuume kwa Mungu na atawala falme zote za dunia. Aidha, anasema maisha
yao hayafungwi na ulimwengu bali wanaalikwa kuishi katika tumaini la kumsubiri Kristu
ajaye. Mpendwa msikilizaji, nasi tunaalikwa pia kukumbuka si watu wa ulimwengu huu
bali tukishafufuliwa na Bwana tunatazama yaliyo ya juu, tunaishi pamoja na Kristu.
Mpendwa,
Bwana anapopaa kuna matukio ambata yanayopaswa kutafakariwa. Kwanza kuna watu wawili
wenye nguo nyeupe, hawa ni wawakilishi wa utakatifu wa Bwana, ni alama ya uwepo wa
Mungu pamoja na Kristu, kumbuka pale kaburini yule aliyekuwa amekalia jiwe! Maneno
waliyoyasema hawa watu wawili ni ujumbe toka kwa Mungu, yafaa na ni lazima kuushika
ujumbe huo. Linatokea wingu, hili latukumbusha safari ya Waisraeli kule jangwani wakitoka
Misri.
Ndiyo kusema waliongozwa na Mungu kwa njia ya wingu, na hivi wingu
ni ishara ya uwepo wa Mungu (Kut.13:22). Mitume na wengine yaani watu wa Galilaya
wanatazama juu na kisha ujumbe unatoka ukiwaambia vivyohivyo alivyokwenda ndivyo atakavyorudi.
Kutazama juu kadiri ya wanamaandiko ni kumwelekea Mungu lakini pia watukumbusha kuhangaikia
upendo hapa duniani ili kutazama kwetu juu kuwe na mzizi wa upendo uliojaa wajibu
wa huduma kwa walio wahitaji.
Mpendwa msikilizaji mwinjili Matayo anatuwekea
mahali pa kukutana Bwana na Mitume kuwa ni Galilaya na si Yerusalemu. Anataka tuelewe
kuwa Mitume walilazimika kuanzia kazi yao ya kitume mahali Bwana alipokuwa ameanzia
utume wake hadharani. Kumbukeni kuwa Galilaya haikuwa inathaminiwa na watu wa Yerusalemu,
lakini Bwana anaithamini na kuipa hadhi akimaanisha kuwa mwanga ni kwa ajili ya wote.
Bwana atakutana na wanafunzi wake pale mlimani, alama ya mlima katika Injili
ya Matayo ni sehemu maalum ambapo Mungu hujidhirisha. Mwinjili Matayo anaonesha jambo
la ajabu kidogo lakini la maana sana akisema “baadhi ya Mitume walikuwa na mashaka”.
Mbona walikukutana na Bwana mfufuka pale Yerusalemu?
Katika hili ataka kutuambia
hivi leo kuwa, hakuna jumuiya iliyo kamilifu, bali mchanganyiko wa wema na wabaya.
Mashaka ya Mitume ni tumaini kwetu maana katika maisha ya imani hatuna uwezo wa kutambua
na kujua kila kitu, isipokuwa kujua kwamba Bwana yu pamoja nasi na ataweza kutanzua
mashaka yetu.
Mpendwa msikilizaji, Bwana anapotoa wajibu kwa Mitume anaweka
pia katika Mitume nguvu au mamlaka ya kutekeleza wajibu huo, ndiyo maana mwanzoni
atasema nimekabidhiwa mamlaka yote na sasa nawatuma enendeni mkafanye. Mamlaka aliyopewa
anawapa Mitume kwa ajili ya kutangaza habari ya wokovu, kumfanya yeye atukuke katika
maisha ya watu. Mamlaka anayowapa ni ya kuwafungulia watu waingie katika Kanisa na
wawe watoto wa Mungu kwa njia ya ubatizo katika UTATU MTAKATIFU.
Mpendwa mwana
wa Mungu, shamrashamra za Kupaa Bwana zinaambatana na wajibu wa kuhubiri injili kwa
kila kiumbe na kwa mataifa tukibatiza katika Utatu Mtakatifu. Na katika kuhubiri,
mwinjili akinukuu maneno ya Bwana anatuhakikishia uwepo wa Bwana pamoja nasi mpaka
ukamilifu wa dahari. Bwana anataka kututoa katika mashaka na wasiwasi unaoweza kujitokeza
katika maisha ya kichungaji wakati Kanisa litakapozaliwa na kuendelea na kazi ya wokovu
wa watu.
Kuwepo kwa Bwana kutokana na tangazo hili ni kiini cha furaha yetu
hivi leo katika Kanisa na ulimwengu wa leo. Bwana kabla ya ufufuko alibanwa na jiografia
yaani katika mazingira ya Israeli, lakini baada ya ufufuko habanwi na mazingira bali
mwanga na furaha kwa mataifa yote.
Mpendwa msikilizaji, ni katika mantiki
hiyo nakualika unaposhangilia Kupaa Bwana uweke nia ya pekee kwa ajili ya kazi ya
kimisionari kwa njia ya sala na majitoleo mbalimbali katika familia na Kanisa kwa
ujumla. Kumbuka wajibu wa kubatiza aliotuachia Bwana yaani kuwajalia watu uzima kama
wajibu msingi na ufunguo mlango wa imani, kumbe kadiri ya taratibu za Kanisa la ulimwengu
na Kanisa mahalia ukaushike vema na hivi Kanisa la Mungu likue na kuzaa matunda.
Mpendwa,
nikutakie furaha na mapendo ukisubiri ujio wa Roho Mtakatifu Dominika ijayo. Tumsifu
Yesu Kristu. Tafakari imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C.PP.S.