2014-05-30 08:08:05

Dumisheni utu na heshima ya binadamu!


Kardinali Thèodore Adrian Sarr, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dakar Senegal, hivi karibuni ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kama kilele cha Jubilee ya miaka 150 ya Kikanisa cha Ngasobil, kilichoko kwenye Seminari ndogo ya Mtakatifu Yosefu, Jimboni humo. RealAudioMP3

Katika mahubiri yake, amewataka wananchi wa Senegal wanapojiandaa kwenye mchakato wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini humo Mwezi Juni, 2014, kuzingatia: haki msingi, utu na heshima ya binadamu. Haya ni mambo msingi ambayo Mama Kanisa anapenda kuyakazia kwa waamini na watu wenye mapenzi mema, ili kukuza amani, utulivu na demokrasia ya kweli.

Haki kadiri ya Maandiko Matakatifu anasema Kardinali Sarr ni utekelezaji wa majukumu ya mtu kadiri ya mapenzi na mpango wa Mungu kwa binadamu. Hapa matendo yanazungumza zaidi kuliko maneno, kwani waswahili husema “maneno matupu hayavunji mfupa”.

Kardinali Sarr amewataka wananchi wa Senegal kusimama kidete kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu hasa katika maeneo ya kazi ambako kuna hatari ya kudhalilisha utu na heshima ya binadamu kwa kutaka kupata faida kubwa. Binadamu ni rasilimali kazi, inayopaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa katika mchakato mzima wa uzalishaji na utoaji huduma kwa jamii.

Ni wajibu kwa wanasiasa kuzingatia kwamba, lengo la kazi ni kumsaidia mfanyakazi kukamilisha utu na heshima yake kama binadamu. Amewataka wanasiasa wanaogombea nafasi mbali mbali za uongozi nchini humo kuibua sera na mikakati inayotekelezeka, ili watakapopata ridhaa ya kuwaongoza wananchi waweze kutekeleza kwa vitendo yale ambayo wanahidi wakati huu wa kampeni za uchaguzi, kwa kuzingatia ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.








All the contents on this site are copyrighted ©.