Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anapoiangalia hija ya kichungaji ya
Baba Mtakatifu Francisko Nchi Takatifu iliyokuwa inaongozwa na kauli mbiu, ili wote
wawe wamoja anasema, Kanisa limeshuhudia nguvu ya imani ikimwilishwa katika uhalisia
wa maisha ya Wakristo.
Kwa mara ya
kwanza Patriaki Bartolomeo wa kwanza alishiriki katika Ibada ya Misa Takatifu, Papa
Francisko alipokuwa anaanza utumishi wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hii ilikuwa
ni nafasi muhimu sana na tukio la kihistoria katika maisha na utume wa Kanisa, kiasi
cha kupanga tena kukutana mjini Yerusalemu, kama kilele cha maadhimisho ya Jubilee
ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana, akazungumza na kusali na Patriaki Anathegoras,
mwanzo wa hija ya majadiliano ya Kiekumene.
Tukio la viongozi hawa wakuu kukutana
na kusali kwa pamoja, Jumapili tarehe 25 Mei 2014, ni tukio la kihistoria, kwani limewahusisha
pia viongozi wa Makanisa mengine ya Kikristo kwa kutambua uzito wa majadiliano ya
kiekumene uliopo mbele yao! Khalifa wa Mtakatifu Petro anapaswa kuwa ni daraja ya
huduma ya umoja, upendo na mshikamano kwa Makanisa ya Kikristo unaojikita kwanza kabisa
katika maisha ya sala! Viongozi wa Makanisa wamesali kwenye Kaburi Takatifu la Yesu
Mfufuka, matendo makuu ya Mungu.
Padre Lombardi anasema, kitendo cha Baba Mtakatifu
Francisko kutoa mwaliko wa kusali pamoja na Rais Mahmoud Abbas wa Palestina na Shimon
Perez wa Israeli ni kuonesha ujasiri unaopata chimbuko lake katika nguvu ya sala!
Baba Mtakatifu alikuwa anatambua uzito wa mwaliko huu, akawa tayari kujitosa kimasomaso
kuwaalika viongozi hawa wawili, si kwa ajili ya kutafuta suluhu ya mgogoro kati ya
Israeli na Palestina, bali kusali kwa pamoja na baada ya hapo, kila mmoja akiongozwa
na dhamiri nyofu aweze kufanya maamuzi magumu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya
Wapalestina na Waisraeli.
Padre Lombardi anasema, amani ambayo ilionekana kuwa
ni jambo lisilowezekana kwa urahisi, Baba Mtakatifu Francisko ameonesha nguvu ya maisha
ya kiroho katika mchakato wa majadiliano yanayopania kutafuta amani, upendo, mshikamano
na mafao ya wengi. Kanisa lina matumaini makubwa kwamba, kwa njia ya sala mambo mengi
yanaweza kubadilika! Ikumbukwe kwamba, amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Papa Francisko ni kiongozi mwenye imani katika neema na baraka kutoka kwa
Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Kanisa lake! Pale ambapo amani inaonekana kuwa ni jambo
lisilowezekana, basi waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanapaswa kuendelea kumwomba
Mwenyezi Mungu ili aweze kuwakirimia amani inayowawajibisha katika vipaumbele vyao!
Padre
Federico Lombardi anasema kwamba, hadi sasa hakuna tarehe maalum iliyopangwa kwa ajili
ya Marais wa Palestina na Israeli kukutana na kusali pamoja na Baba Mtakatifu Francisko
mjini Roma. Ni matumaini ya Padre Lombardi kwamba, Marais hawa wawili ambao wameonesha
kuridhia ombi na mwaliko kutoka kwa Baba Mtakatifu watapanga tarehe ya kukutana na
kusali kwa pamoja. Waamini na watu wenye mapenzi mema, wanaweza kuendelea kusali kwa
ajili yakufanikisha tukio hili la kihistoria kwa ajili ya kuombea amani.
Padre
Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, hija ya kichungaji ya
Baba Mtakatifu Francisko ilisheheni matulio makubwa katika maisha na utume wa Kanisa.
Licha ya Baba Mtakatifu na wale waliokuwa katika msafara wake kuchoka, lakini imekuwa
ni chemchemi ya furaha, imani na matumaini kwa ajili ya mafao ya wengi: Baba Mtakatifu
ametenda yote kadiri ya uwezo wake, Padre Lombardi anasema, bila shaka alikuwa ametunza
akiba mahali fulani, hapa si bure!
Imeandaliwa na Padre Richard A. Mjigwa.
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.