2014-05-27 14:38:29

Asante sana Bikira Maria!


Baba Mtakatifu Francisko baada ya kurejea mjini Vatican ili kuendelea na maisha na utume wake kama kawaida, mapema asubuhi siku ya Jumanne, tarehe 27 Mei 2014 amekwenda kutembelea Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu lililoko mjini Roma, kumshukuru Bikira Maria kwa ulinzi na maombezi yake wakati wa hija yake ya kitume Nchi Takatifu.

Baba Mtakatifu ameyaweka matunda yatakayopatikana baada ya hija hii ya kitume chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria. Baada ya kuwasili, amepokelewa na viongozi wa Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu na kusali kwa kitambo na baadaye kuweka shada la maua kwenye Sanamu ya Bikira Maria.

Baba Mtakatifu amesalimiana na mahujaji pamoja na waamini waliokuwa kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria huku akionesha furaha kubwa moyoni mwake kwa kuhitimisha hija ya kichungaji iliyomwezesha kutembelea maeneo matakatifu na kukutana na waamini wa dini mbali mbali kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano kati ya watu!

Hii ni mara ya tisa kwa Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi cha mwaka mmoja tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kutembelea Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu!







All the contents on this site are copyrighted ©.