2014-05-25 12:12:44

Watoto wanastahili kupokelewa, kutunzwa na kusaidiwa!


Baba Mtakatifu Francisko akiwa mjini Bethlehemu, Jumapili tarehe 25 Mei 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu katika Uwanja wa Pango la Mtoto Yesu mjini Bethlehemu, maarufu kama "nyumba ya mkate". Baba Mtakatifu katika mahubiri yake, ametafakari kwa kina kuhusu Fumbo la Umwilisho. Amewashukuru viongozi wa Serikali na Kanisa, familia ya Mungu nchini Palestina pamoja na watu wote wenye mapenzi mema wanaojisadaka kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, imani, matumaini na mapendo yanaendelea kustawi na kushamiri kati ya watu!

Yesu Kristo aliyezaliwa mjini Bethlehemu ni alama wazi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa watu waliokuwa wanasubiri wokovu. Ameendelea kuwa ni kielelezo makini cha upole na uwepo wa Mungu duniani. Mtoto Yesu kama walivyo watoto wengine wote duniani ni alama ya matumaini, maisha na utu. Ni kielelezo cha taifa, jamii na dunia inayothamini tunu msingi za maisha ya familia. Mambo haya yanawezekana pale tu, watoto wanapopokelewa, wanapopendwa, wanapolindwa na kuthaminiwa, hapo kwa hakika familia inaweza kushamiri. Baba Mtakatifu anaipongeza taasisi ya Effeta ya Paulo VI inayohudumia watoto viziwi kutoka Palestina!

Mtoto Yesu kama walivyo watoto wengine wote anasema Baba Mtakatifu ni dhaifu, anahitaji kusaidiwa na kutunzwa, changamoto ya kuwapokea na kuwalinda watoto tangu wanapotungwa mimba tumboni mwa mama zao. Lakini inasikitisha kuona kwamba, kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuna watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi pembezoni mwa miji mikuu au vijijini. Ni watoto wanaonyanyaswa na kudhulumiwa; wanaofanyishwa kazi za suluba au kuzamishwa maji huko kwenye Bahari ya Mediterania. Haya yote ni matendo ya aibu sana mbele ya Mwenyezi Mungu, aliyejifanya Mtoto.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuiga mfano wa Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu waliomlinda na kumtunza Mtoto Yesu dhidi ya ukatili wa Herode! Waige mfano wa wachungaji kutoka kondeni waliokwenda kumwabudu Mtoto Yesu. Kimsingi watu wajenge utamaduni wa kusikiliza, kuwalinda na kusali kwa ajili ya watoto. Kilio cha watoto, kiashe dhamiri za watu kuwahudumia kwa upendo, kwa kuguswa na mahitaji ya watu wanaokufa kwa njaa duniani wakati ambako sehemu nyingine za dunia watu wanakula na kusaza. Watoto wapewe huduma bora za tiba, kwa kuwalinda na kuondokana na biashara haramu ya silaha inayowanyanyasa watoto kwa kuwapeleka vitani au kuwafanyisha kazi ngumu.

Baba Mtakatifu anahitimisha mahubiri yake kwa kusema, kila mtoto anayezaliwa duniani kama ilivyokuwa kwa Mtoto Yesu anapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa na familia, jamii na ulimwengu katika ujumla wake. Huu ni mwaliko wa kuwa na mwelekeo mpya wa maisha unaojikita katika mahusiano mema pasi na kinzani, vita, ulaji wa kupindukia. Watu wajitahidi kujenga mahusiano ya kidugu, kwa kusameheana, kujipatanisha pamoja na kushirikishana tone la upendo!







All the contents on this site are copyrighted ©.