2014-05-25 07:44:06

Biashara haramu ya silaha ni chanzo cha vita na mahangaiko ya watu!


Baba Mtakatifu Francisko baada ya kuwasili nchini Yordani, akapata nafasi ya kuzungumza na wenyeji wake, akaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Michezo wa Kimataifa mjini Amman, jioni alitembelea eneo la Bethania ng'ambo ya mto Yordan, mahali alipobatizwa Yesu. Hapo alipata nafasi ya kusali kwa ukimya.

Baadaye, Baba Mtakatifu Francisko alikutana na wakimbizi pamoja na vijana walemavu, kwenye Kanisa ambalo Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliweka jiwe lake la msingi kunako mwaka 2009. Baba Mtakatifu alipata nafasi ya kusikiliza shuhuda mbali mbali zilizotolewa na wakimbizi pamoja na walemavu hao!

Baba Mtakatifu katika hotuba yake amesema, kwa makusudi kabisa aliamua kukutana nao ili kuweza kuuona uso wa Yesu Msulubiwa na upendo wake unaowakirimia wanadamu utu na wokovu. Baba Mtakatifu amewashukuru viongozi wa Serikali nchini Yordan, wananchi na Mashirika ya misaada ya Kanisa Katoliki yanayotekeleza utume wake miongoni mwa wakimbizi bila ubaguzi. Hiki ni kielelezo cha huruma ya Yesu.

Baba Mtakatifu kwa mara nyingine tena anaiomba Jumuiya ya Kimataifa kusaidia mchakato wa kuleta amani na upatanisho wa kitaifa nchini Syria. Anawahimiza vijana kujitosa kimasomaso kushiriki katika ujenzi wa jamii inayojikita katika msingi wa haki na heshima kwa maskini! Watu wanapenda amani, lakini bado kuna watu wanaotaka kujitajirisha kwa kuchochea chuki, ghasia na vita ili kukuza soko la biashara haramu ya silaha. Baba Mtakatifu anawaalika wote wanaojihusisha na biashara haramu ya silaha, kutubu na kuongoka, ili kweli waweze kuwa ni vyombo vya ujenzi wa amani.

Baba Mtakatifu Francisko anaiomba Jumuiya ya Kimataifa kuonesha ushirikiano wa dhati na Yordan katika kuwapokea na kuwahudumia wakimbizi pamoja na kuendeleza harakati za ujenzi wa amani nchini Syria kwa kusitisha vita na kuheshimu utu wa binadamu pamoja na kutoa msaada kwa wahanga wa kinzani hizi za kijamii. Mtutu wa bunduki kamwe hauwezi kuwa ni suluhisho la matatizo ya wananchi, kumbe kuna haja ya kuwa na mwelekeo mpya unaojikita katika majadiliano, kwa kuguswa na mahangaiko ya watu wanaoteseka, sanjari na kutafuta suluhu ya kisiasa kwa kuwajibika zaidi.

Mwishoni, Baba Mtakatifu amewataka vijana na walemavu kujiunga naye kwa ajili ya kusali ili kuombea amani, kwa kutolea shida na mahangaiko yao mbele ya Mwenyezi Mungu, kwani kwa njia hii, kweli sala zao zinakuwa na thamani kubwa. Anawataka vijana kujibidisha katika ujenzi wa jamii inayoheshimu na kuthamini wanyonge, wagonjwa, watoto na wazee. Hata katika shida na mahangaiko ya ndani, kamwe wasikate tamaa, watambue kwamba, wako mbele ya Mungu na daima anawakumbuka katika sala na sadaka yake!







All the contents on this site are copyrighted ©.