2014-05-24 10:02:27

Papa Francisko aanza hija yake ya kichungaji Nchi Takatifu


Baba Mtakatifu Francisko ameondoka mjini Roma asubuhi, tarehe 24 Mei 2014 tayari kwa hija ya kitume huko Yordani, Palestina na Israeli kama kilele cha maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana, akazungumza na kusali pamoja na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu, huu ukawa ni mwanzo mpya wa mchakato wa majadiliano ya kiekumene.

Baba Mtakatifu katika Uwanja wa ndege wa Fiumicino, Roma amesindikizwa na viongozi mbali mbali wa Kanisa na Serikali ya Italia. Ametumia nafasi hii kuwasalimia mmoja mmoja na kuwatakia kheri na baraka. Kama desturi, Baba Mtakatifu alibeba mkoba wake mweusi tayari kuanza safari ya kitume Nchi Takatifu.

Baba Mtakatifu amewaandikia wakuu wa Nchi ya Italia, Ugiriki, Cyprus na Israeli ujumbe wa matashi mema wakati alipokuwa anasafiri kuelekea mjini Amman, kituo cha kwanza cha hija yake ya kitume! Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe aliomwandikia Rais Giorgio Napolitano wa Italia, anamwambia kwamba, anaelekea Nchi Takatifu ili kuadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na Patriaki Anathegoras wa Yerusalem pamoja na kusali kwa ajili ya kuombea haki, amani pamoja na kukoleza majadiliano ya kiekumene na kidini. Anawatakia kheri na baraka wananchi wa Italia, anawaomba pia kumkumbuka katika sala zao.

Naye Rais Giorgio Napolitano wa Italia amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko na kwamba, Jumuiya ya Kimataifa ina matumaini makubwa katika hija hii ya kitume huko Nchi Takatifu, mahali ambapo kuna kinzani kubwa katika historia yake na ulimwengu kwa ujumla. Ni matumaini ya Rais Napolitano kwamba, hija hii itakuwa ni cheche za matumaini kwa wale wanaotaka kusimama kidete kuendeleza amani na utulivu. Rais Napolitano anamtakia mafanikio mema katika hija hii ya kitume.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Rais Karolos Paoulias wa Ugiriki anamtakia mafanikio mema katika kukuza na kudumisha misingi ya haki na amani, anawaombea baraka tele kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko akimwandikia Rais Nicos Anastasides wa Ugriki anasema, anawatakia kheri na baraka tele wananchi wa Ugiriki na kwamba, anawaombea furaha na amani kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko amemwandikia pia ujumbe Rais Shimon Peres wa Israel kwa kumtakia matashi mema na wananchi wote wa Israeli na kwamba, ana matumaini ya kukutana naye Nchi Takatifu wakati wa hija yake ya kichungaji. Anawatakia wote baraka tele!







All the contents on this site are copyrighted ©.