Padre Mario Vergara na Katekista Isidore Ngei Ko Lat watangazwa kuwa wenyeheri!
Kardinali Angelo Amato, Rais wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri
na watakatifu, katika maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria msaada wa Wakristo inayoadhimishwa
kila mwaka ifikapo tarehe 24 Mei, amewatangaza Watumishi wa Mungu Padre Mario Vergara,
Mwanashirika kutoka Taasisi ya Kipapa ya utume wa nje, PIME, Italia na Katekista Isidore
Ngei Ko Lat kutoka Burma kuwa Wenyeheri. Wenyeheri hawa wapya waliuwawa kikatili kutokana
na chuki za kiimani kunako mwaka 1950 nchini Burma.
Ni matumaini ya Mama Kanisa
kwamba, ujasiri na ushujaa wa imani ulioneshwa na Wenyeheri hawa wapya, utakoleza
ari na moyo wa kimissionari hususan miongoni mwa Makatekista, wanaoendelea kujisadaka
kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa hasa katika Nchi za Kimissionari. Kanisa linawashukuru
kwa sadaka na majitoleo yao.
Mwenyeheri Padre Mario Vergara alizaliwa mjini
Frattamaggiore kunako mwaka 1910. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapewa
Daraja takatifu la Upadre tarehe 28 Agosti 1934. Alitekeleza maisha na utume wake
wa Kipadre katika mazingira magumu na hatarishi, akasaidiwa na Makatekista. Wakati
wa Vita kuu ya Pili ya Dunia kunako Mwaka 1941, akakamatwa na kufungwa kwenye kambi
ya Waingereza nchini India, ambako alitumikia kifungo kwa muda wa miaka 4.
Alipoachiliwa
huru alirudi nchini Italia na baadaye akakata shauri ya kurudi nchini Burma kuendelea
na utume wake, akaona Burma ikijipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza kunako mwaka
1948. Lakini baada ya muda mfupi Burma ilijikuta inatumbukia katika machafuko ya kisiasa
na kijamii, Padre Mario Vergara, akajitokeza kuwa ni sauti ya wanyonge, kiasi cha
kuchukiwa na waasi wa Serikali ya Burma.
Tarehe 24 Mei 1950 wakati Padre Vergara
na Katekista Isidore Ngei Ko Lat walipokwenda kuomba kuachiliwa kwa Katekista mmoja
aliyekuwa amekamatwa na kufungwa gerezani walikutana na kiongozi wa waasi, baada ya
kuwahoji sana, akaamuru watiwe pingu na hatimaye kuuwawa kikatili. Miili yao iliyofungwa
kwenye mfuko na kutupwa mtoni.
Katekista Isidore Ngei Ko Lat, anakuwa ni mwamini
wa kwanza kabisa katika historia ya Kanisa Katoliki nchini Burma kutangazwa kuwa Mwenyeheri.
Yeye alibatizwa tarehe 7 Septemba 1918. Ni kijana aliyekulia katika mazingira ya Kanisa,
akawasaidia Wamissionari katika utume wao. Akajiunga na Seminari ndogo huko Toungoo,
akaonesha ari na moyo wa kutaka kuwa Padre, lakini afya yake ilikuwa mbaya, kiasi
cha kumfanya kushindwa kuendelea na masomo. Lakini aliendelea kujisadaka kwa ajili
ya Kristo na Kanisa lake kama mwamini mlei, bila kuoa, akafunga shule binafsi, mahali
ambapo alifundisha Katekesi.
Kunako mwaka 1948 akakutana na Padre Vergara
aliyemwalika kufundisha Katekesi mjini Shadaw. Mama Kanisa anawashukuru kwa majitoleo
yao, leo hii wameandikwa kwenye orodha ya Wenyeheri ndani ya Kanisa.