2014-05-24 17:19:25

Kuna watu wenye mapenzi mema wanaotaka kuona amani ikitawala duniani!


Mfalme Abdalla wa Pili wa Yordan amemkaribisha Baba Mtakatifu Francisko nchini mwake kwa kumwambia kwamba, dunia inakabiliana na changamoto mbali mbali zinazotokana na watu kutoaminiana na kutokubali mabadiliko wala kuheshimiana. Yordan ni nchi ya watu wenye imani thabiti. Anasema kuna haja ya kuunganisha sauti za watu wote wenye mapenzi mema, ili kuheshimiana, kujenga na kudumisha amani pamoja na uchaji wa Mungu bila kusahau majadiliano ya kidini.

Mfalme Abdalla anasema duniani bado kuna watu wenye mapenzi mema wanaopenda kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; amani na utulivu. Anamshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwa ni mfano bora wa kuigwa katika kutetea haki msingi za binadamu pamoja na kuendeleza majadiliano ya kidini, ili kujenga daraja la amani, kama ilivyo pia kwa Yordan.

Anasema, nchi yake inaendelea kuhimiza umuhimu wa kujenga jamii inayosimikwa katika msingi wa amani na utulivu, huruma na haki kwa kuwakata watu wanaotaka kujenga chuki na uhasama kati ya watu, bali kudumisha amri ya upendo kwa Mungu na jirani. Anapenda kuiona dini ya Kiislam ikijisimika katika amani na utulivu. Anampongeza Papa Francisko kwa kutembelea Mto Yordan mahali alipobatizwa Yesu. Yordan itaendelea kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema katika ujenzi wa misingi ya haki, amani na utulivu, ili kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika maisha ya mwanadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.