2014-05-24 16:41:43

Hotuba ya Papa kwa viongozi wa Serikali ya Yordan!


Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kuwasili mjini Amman, Jumamosi mchana 24 Mei 2014 alimtembelea Mfalme Abdallah wa pili pamoja na familia yake baadaye amekutana na kuzungumza na viongozi wa Serikali kwenye Ikulu ya Mfalme. Baba Mtakatifu amemshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumpatia fursa ya kutembelea Yordan akifuata nyayo za watangulizi wake Papa Paulo VI, Yohane Paulo II na Benedikto XVI.

Anakumbuka mkutano wao wa pamoja uliofanyika mjini Vatican hivi karibuni. Anasema, Yordan ni nchi ambayo ina utajiri mkubwa wa kidini kutokana na uwepo wa dini ya: Kiyahudu, Kikristo na Kiislam. Ni nchi ambayo imeonesha ukarimu mkubwa kwa wakimbizi kutoka Palestina, Iraq na maeneo ambayo bado kuna vita na kinzani za kijamii kama vile Syria. Ukarimu huu unapaswa kuheshimiwa na kuungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa. Kanisa Katoliki kadiri ya uwezo wake, linapenda kuendelea kutoa huduma kwa wakimbizi na wahitaji kwa kutumia Shirika la Misaada la Caritas, Yordan.

Baba Mtakatifu anasikitishwa na vita pamoja na kinzani zinazoendelea huko Mashariki ya Kati, anapenda kuchukua fursa hii kuwashukuru viongozi wa Yordani kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kutafuta amani ya kudumu katika Ukanda huu na kwamba, kuna haja ya kuhakikisha kwamba, suluhu ya kudumu inapatikana nchini Syria sanjari na mgogoro kati ya Israeli na Palestina.

Baba Mtakatifu anaishukuru Jumuiya ya Waislam chini ya uongozi wa Mfalme Abdalla II kwa kuendeleza tunu msingi za mafundisho ya dini ya Kiislam zinazojikita katika amani na utulivu kati ya waamini wa dini mbali mbali. Anaipongeza Serikali kwa kuanzisha majadiliano ya kidini na uelewano mwema kati ya Wayahudi, Waislam na Wakristo sanjari na kushiriki katika juma la utulivu kati ya dini, ililoanzishwa na Umoja wa Mataifa.

Baba Mtakatifu anaishukuru na kuipongeza Jumuiya ya Kikristo ambayo imeendelea kushiriki katika kuchangia mafao ya wengi ndani ya Jamii na hata katika uchache wao, wamekuwa na mchango mkubwa katika sekta ya elimu na afya, huduma ambazo zinatolewa bila ubaguzi na watu wanaendelea kuungama imani yao katika hali ya utulivu, huku wakiheshimu uhuru wa kidini, msingi wa haki zote za binadamu.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, haki hii itaheshimiwa katika Ukanda wa Mashariki ya Kati kwa mtu binafsi au kundi la watu. Wakristo wanajisikia kuwa ni sehemu ya raia wa Nchi zao na wanataka kushiriki kikamilifu katika mchakato wa ujenzi wa jamii kwa kushirikiana na waamini wa dini ya Kiislam, kwa kutoa mchango wao wa dhati.

Baba Mtakatifu anawatakia wananchi wa Yordan amani na maendeleo na kwamba, hija hii ya kitume isaidie mchakato wa kutafuta na kuendeleza mahusiano mema kati ya Wakristo na Waislam. Mwishoni, Baba Mtakatifu amemtakia Mfalme Abdallah wa Pili maisha marefu na baraka tele!







All the contents on this site are copyrighted ©.