2014-05-23 11:41:46

Utajiri wa maisha ya kiroho Yordan!


Baba Mtakatifu Francisko anaianza hija yake ya kitume kwa kutembea Amman nchini Yordan. Hapa kuna mambo makuu matatu ya kukumbuka: hapa kuna changamoto ya kimissionari, kinabii na chemchemi ya maisha ya Kikristo.

Padre Samir Khalid Samir anasema, Yordan ni mahali ambapo watu kutoka katika tamaduni, lugha na jamaa wanakutana, kumbe, ni sehemu muhimu sana katika kudumisha utamaduni na misingi ya maisha ya Kiristo huko Mashariki ya Kati, hali ambayo wakati mwingine inasababisha kinzani na migongano ya kijamii. Ni jukumu la Wakristo na Waamini wa dini mbali mbali kudumisha majadiliano ya kiekumene na kidini, ili haki, amani na utulivu viweze kutawala!

Majiundo makini: kiroho, kimwili na kiakili yatawasaidia waamini kuweza kufahamiana, kupendana na kushikamana kama ndugu, ili kuondokana na falsafa na kinzani zilizojitokeza katika historia ya watu wanaoishi huko Nchi Takatifu, ndiyo maana Kanisa limewekeza kwa kiasi kikubwa katika Chuo Kikuu cha Madaba, ili vijana wajifunze utamaduni wa kuheshimiana na kuthaminiana, kwani wao ndio tegemeo la jamii katika ujenzi wa misingi ya haki, amani na utu na umoja, kama alivyosema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI wakati anaweka jiwe la msingi katika ujenzi wa Chuo Kikuu cha Madaba.

Utu na heshima ya binadamu ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kukazia pia uhuru wa kidini.

Hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko inapania pamoja na mambo mengine kuimarisha ari na mwamko wa kimissionari miongoni mwa Wakristo wanaoishi Nchi Takatifu, kwani wao ni mashahidi wa mambo yale ambayo waliyasikia, wakayaona na kuyashuhudia katika maisha, kwani Fumbo la Pasaka ni kiini cha imani na matumaini ya Watu wa Mungu. Kwa kifo na ufufuko wake, Yesu amemkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.









All the contents on this site are copyrighted ©.